Mvulana wa miaka mitatu na nusu alifariki baada ya moto kuzuka katika nyumba yao ya kupanga katika eneo la Kwa Mashariki, Kaunti Ndogo ya Mwingi Kati, huko Kitui. Polisi waliarifiwa Jumanne, na maafisa waliotembelea nyumba hiyo waligundua kuwa chumba kimoja cha nyumba hiyo kilikuwa kimeshika moto, kikiunguza kitanda, godoro na matandiko mengine. Kulingana na mamake mtoto huyo, alifunga nyumba na kumwacha mvulana huyo peke yake yapata saa nane mchana. Alirudi yapata saa kumi na moja jioni na kukuta kitanda na matandiko yakifuka moshi, huku mwanawe akiwa amelala bila fahamu, kwenye godoro la ziada lililokuwa sakafuni.