Kenya imeimarisha maandalizi ya mvua kubwa inayoweza kutokea Oktoba-Novemba-Disemba, huku Kituo cha Kitaifa cha Operesheni za Majanga kikikadiria kwamba takriban watu milioni 1.5 wanaweza kuathiriwa na wengine elfu 500 kuhama makaazi yao chini ya hali mbaya zaidi. Onyo hilo limetolewa wakati Jukwaa la 13 la Kitaifa la Mtazamo wa Hali ya Hewa likifunguliwa katika hoteli ya Nairobi, likiwakutanisha mashirika ya serikali, wataalamu wa hali ya hewa, mashirika ya kibinadamu, washirika wa maendeleo, sekta binafsi na mashirika ya kiraia ili kupanga kwa mvua inayotarajiwa. Mkurugenzi wa kituo hicho David Samoei, alisema nchi sasa inajikita katika kujiandaa kwa athari zinazowezekana za mvua badala ya kujadili kama zitatokea.