Wapelelezi wameanzisha msako wa mshukiwa wa miaka 18 anayetuhumiwa kumdunga kisu kijana mwenzake katika eneo la Dandora jijini Nairobi. Kulingana na polisi, shambulio hilo lilitokea usiku wa jumatano karibu na lango katika eneo la Canaan. Tukio hilo liliripotiwa katika Kituo cha Polisi cha Dandora na mamake, ambaye aliwaambia maafisa kwamba mwanawe alikuwa amedungwa kisu kifuani. Maafisa wa polisi waliofika eneo la tukio walibaini kuwa mwathiriwa, Kelvin Karanja, alikuwa amedungwa kisu kifuani na mvulana mwingine chini ya hali ambazo bado zinachunguzwa.