Baraza la makanisa nchini NCCK limewaonya wanasiasa dhidi ya kuwatumia vibaya vijana wasio na ajira kwa vurugu za kisiasa kabla ya uchaguzi wa 2027. Mwenyekiti wa Kanda ya Pwani ya NCCK Askofu Peter Mwero alisema ugumu wa kiuchumi umewaacha vijana wengi katika hatari ya kudanganywa kupitia kupewa pesa na kuajiriwa katika shughuli za kisiasa zenye kuvuruga amani. Aliwasihi vijana kukataa vurugu, kujiandikisha kama wapiga kura na kushiriki kwa amani katika mchakato wa kidemokrasia.