
RAIS William Ruto amefichua jinsi mpango wa bima ya kitaifa SHA unavyozidi kupata uungaji mkono na Imani kuu kutoka kwa Wakenya.
Akizungumza na Wakenya wanaoishi nchini China, rais Alifichua kwamba SHA inazidi kuboreka kila siku huku akifichua kwamba huwa anapokea taarifa za takwimu za SHA kila siku kutoka kwa mamlaka husika.
Kiongozi wa nchi alibainisha kwamba jana alipokea takwimu zikionyesha kwamba jumla ya wakenya takribani elfu 55 walijiandikisha kwenye SHA kwa siku hiyo pekee.
Rais alisema kwamba kwa kila siku, wastani wa Wakenya wanaojisajili kwenye SHA ni kati ya 45,000 hadi 60,000, akipongeza Wakenya kwa kuonyesha Imani yao kwa bima hiyo mpya.
“Tumenanzisha mpango wa huduma ya afya kwa wote ambayo aghalabu inajulikana kama Taifa Care ama SHA. Na nilikuwa naangalia kwa takwimu usiku wa jana, huwa napata ripoti kila siku majira ya saa nne usiku.”
“Jana Wakenya 55,000 walijiandikisha kwa SHA. Kwa wastani, kila siku wakenya kati ya 45,000 na 60,000 hujiandikisha kwenye SHA,” rais alieleza.
Alisema kwamba SHA ni bima bora kwani inanufaisha kila mtu hadi wale watu ambao hawajawahi kuwa chini ya bima yoyote ya afya katika maisha yao.
“Kwa mara ya kwanza watu ambao hawajawahi kuwa na bima yoyote ya afya sasa wanapata huduma ya bima ya afya. Kwa miaka ya nyuma, NHIF ilikuwa imetengwa mahususi kwa watu ambao ama wana mshahara au wenye walikuwa katika nafasi ya kulipia.”
“Lakini safari hii tumeanzisha huduma ya afya kwa wote, jambo ambalo kwa muda mrefu tulikuwa tunataka kufanya. Nakumbuka serikali ya NARC ilitaka kulifanya, na pia nakumbuka tulijaribu kulifanya katika serikali ya Jubilee, na hatukuweza kufanikiwa. Lakini najivunia kwamba safari hii tuliweza kufanikisha,” Ruto aliongeza.
Rais Alifichua kwamba mpango wa kuzindua SHA ulichukua mchakato wa maandalizi kwa kipindi cha takribani miaka 2.
“Tulichukua takribani miaka 2 ya kupanga na kutengeneza mfumo sahihi na leo hii ninaweza sema kwa ujasiri kwamba kinyume na NHIF ambayo ilikuwa na karibia watu milioni 7 waliojisajili, leo tuna watu milioni 21 waliojisajili kwenye SHA,” rais Ruto alikariri.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!