Linda Kiome

Njuri Ncheke, Baraza la Wazee wa Meru limekaribisha uteuzi wa wakili Linda Kiome kama Naibu Gavana mpya wa Kaunti ya Meru. 

Wazee hao walisema uteuzi huo ni dhibitisho kwamba watu wa Meru hawachukii wanawake kama ilivyosawiriwa katika kuondolewa kwa gavana wa kwanza mwanamke wa kaunti hiyo - Kawira Mwangaza. 

Katika kikao na wanahabari siku ya Jumamosi, Njuri Ncheke aliwataka Wakenya kukomesha simulizi kwamba jamii hiyo ina mielekeo ya kihuni ya wanaume. Wazee walisema wanawake wanaheshimika katika jamii. 

"Hii ni dhibitisho kwamba watu wa Meru wanapenda wanawake, hatupigani na wanawake.  Tulichokosa ni uongozi bora. Hata kama angekuwa mwanamume na hawana uongozi mzuri, tungefanya kama tulivyofanya kwa aliyekuwa (Kawira)," alisema mwanachama wa Njuri Ncheke Jasphat Murangiri.

Baada ya kuapishwa kwa naibu wake Isaac Mutuma, Mwangaza alitoa hotuba kwa wanahabari, ambapo alilaumu unyanyasaji wa kiume kwa kushtakiwa kwake. 

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Mwangaza alidai kuwa alikabiliwa na vita vikali kutoka kwa wapinzani wake ambao  walikataa kuwakubali wanawake katika uongozi. 

Aliongeza kuwa kushtakiwa kwake hakukutokana na matakwa ya wananchi bali ni hatua iliyochukuliwa na washindani wake ambao walishirikiana na Serikali ya Kitaifa kumhakikishia kuondoka kwake.

"Leo, navunja ukimya wangu kushughulikia dhuluma kubwa niliyokumbana nayo kama kiongozi mwanamke katika jamii yenye mfumo dume," alibainisha. 

"Kushitakiwa kwangu hakukuwa onyesho la utendakazi au uadilifu wangu bali ni hatua iliyohesabiwa ya wababe wanaume, washindani wa kisiasa, na kwa manufaa ya kisiasa, Serikali ya Kitaifa iliyojitolea iliyo tayari kumnyamazisha mwanamke ambaye alithubutu kuongoza."

Gavana huyo wa zamani alirejelea jinsi wapinzani wake walivyokuwa wakishangilia kwa majigambo wakati wa hafla ya kuapishwa kwa gavana mpya Isaac Mutuma, akiashiria kuwa shughuli hiyo yote ilikusudiwa kukandamiza utawala wa wanaume katika uongozi wa Kaunti ya Meru.

"Ni ukweli wa kusikitisha kwamba mwaka wa 2025, viongozi wanawake bado wanabaguliwa kimfumo, kunyanyaswa, na kutengwa. Kesi yangu ni ukumbusho tosha wa vikwazo ambavyo wanawake wanakumbana navyo katika siasa na urefu ambao baadhi wataenda kudumisha hali iliyopo," aliongeza.

Mwangaza alipoteza wadhifa wake baada ya mijadala mitatu ya kuondolewa katika Seneti.

Azma yake ya kuzuia kuondolewa afisini ilififia Machi 14 baada ya Mahakama Kuu kuamua kuwa Seneti ilitenda kulingana na Katiba wakati wa mchakato wa kuondolewa kwa Mwangaza.

Mahakama ilitupilia mbali madai yake kwamba mashtaka hayo yalikumbwa na kasoro, ikisema kwamba alishindwa kutoa ushahidi wa kutosha kuunga mkono madai yake.