TAKRIBAN $53m (£43m) katika madai ya fedha haramu zilizopatikana kutoka kwa waziri wa zamani wa mafuta wa Nigeria Diezani Alison-Madueke miongoni mwa zingine zitatumika kufadhili huduma za umma, wizara ya sheria ya nchi hiyo inasema.


Pesa hizo zinarejeshwa Nigeria kutoka Marekani, ambayo mamlaka yake inadai kuwa waziri wa zamani wa mafuta, Alison-Madueke alijitajirisha yeye na wengine, huku akiongoza kampuni ya mafuta ya serikali ya Nigeria kwa kutoa kandarasi badala ya rushwa.


Marekani ilidai kuwa pesa hizo zilitumika kununua boti kubwa la urefu wa mita 65 liitwalo Galactica Star pamoja na mali nyingi za kifahari huko California na New York.


Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Alison-Madueke, 64, amekuwa akikana madai yote ya kufanya makosa.


Mafanikio yake yanayodaiwa kupatikana kwa njia haramu pia yanachunguzwa nchini Uingereza, ambapo miaka miwili iliyopita alishtakiwa kwa makosa ya hongo ikiwa ni pamoja na zawadi za bidhaa za kifahari za Louis Vuitton, malipo ya karo za shule za kibinafsi, na angalau $ 127,000 taslimu.


Mhusika mkuu katika utawala wa Rais wa zamani Goodluck Jonathan, pia aliwahi kuwa rais wa kwanza mwanamke wa kundi la wasafirishaji mafuta la Opec.


Wakati wake kama waziri wa rasilimali za petroli wa Nigeria ulianza mwaka 2010 na kumalizika mwaka 2015. Hapo awali aliwahi kuwa waziri wa uchukuzi, na waziri wa madini imara na maendeleo ya chuma.


Wizara ya Sheria ya Marekani ilitangaza mwaka 2023 maazimio ya mwisho ya kesi mbili za madai juu ya kutaifishwa kwa mali ambazo ziliripotiwa kufukuzwa nchini na kupitia Marekani na Alison-Madueke na washirika wake.


Siku ya Ijumaa, Marekani na Nigeria zilithibitisha kuwa kiasi cha $52.88m kitarejeshwa katika taifa hilo la Afrika Magharibi.


Hii itakuwa ni mara ya kwanza kurejeshwa nchini Nigeria kwa mali nje ya nchi hiyo ya Afrika Magharibi inayohusishwa na Alison-Madueke, shirika la habari la Reuters linaripoti.


Akizungumza katika hafla ya utiaji saini rasmi katika mji mkuu wa Nigeria, Abuja, Mwanasheria Mkuu na Waziri wa Sheria, Lateef Fagbemi, alisema kurejeshwa kwa fedha hizo kunaashiria hatua kubwa katika juhudi zinazoendelea za kupambana na rushwa.


Fagbemi alisema $50m ya pesa hizo zitapitia Benki ya Dunia kusaidia miradi ya usambazaji wa umeme vijijini, na $2.88m iliyobaki itaelekezwa kwa Taasisi ya Kimataifa ya Haki ili kuimarisha mfumo wa haki na kukuza juhudi za kupambana na ufisadi.


 


Wakati huo huo Balozi wa Marekani nchini Nigeria, Richard Mills, amesisitiza haja ya uwajibikaji pamoja na ufuatiliaji makini wa fedha zinazorejeshwa.


 


"Wizara ya sheria lazima ihakikishe kuwa fedha hizi zinatumika kwa uwazi na ipasavyo kuboresha maisha ya Wanigeria," alisema.


 


Mnamo Novemba 2022, serikali ya Marekani ilirejesha Nigeria, $20.6m katika mali inayodaiwa kuibwa na kiongozi wa zamani wa jeshi la Nigeria Jenerali Sani Abacha.


 


Miaka mitano iliyopita, Washington ilihamisha $311.8m kwa serikali ya Nigeria kama sehemu ya makubaliano ya awali ya kurejesha mali ambayo yalianzia utawala wa Abacha.