Aliyekuwa naibu wa rais, Rigathi Gachagua amefichua kwamba maisha yake yamekuwa yakiendelea kwa njia nzuri tangu kubanduliwa kwake.

Akipuuzilia mbali uwezekano owote wa kuzama kwenye bahari ya mawazo baada ya kupoteza kazi yake kama naibu wa rais, Gachagua alisema kwamba kwa sasa yeye yuko vizuri kabisa, akiwashukuru Wakenya kwa kumuombea.

Mwanasiasa huyo alikuwa anazungumza JUmapili katika ibada kaunti ya Kajiado ambapo alisema hata yeye ni kama rais mstaafu Uhuru Kenyatta ambaye alisema Jumamosi kwamba hana mambo mengi kwani anaangalia runinga na kusikiliza redio kama Wakenya wengine tu.

“Mimi sina maneno mengi, yangu tu ni kusema ahsante sana. Ningependa kuwashukuru watu wa Kajiado ya Kaskazini kwa maombi yenu. Na mimi sina stress, mimi nime’relax vizuri sana. Sasa hakuna mtu ananilaumu kwa ile shida iko Kenya, wengine walaumiwe, wajibu,” Gachagua alisema.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

“Mimi ni mtu sasa wa kuangalia. Hata Uhuru Kenyatta, rais wetu alisema yeye yake ni kuangalia kwa TV na kusikiliza kwa redio. Hata mimi naangalia Tv na kusikiliza redio. Wacha wale wanaendesha walaumiwe,” Gachagua aliongeza.

Kiongozi huyo hata hivyo aliwarai wananchi kuwaheshimu viongozi wao, akilenga mkuki kwa serikali ya Ruto kwamba kama yeye ndiye alikuwa shida sasa shida inafaa kuwa imeisha baada ya kumbandua.

“Acha tusubiri tuone jinsi hali inavyokuwa. Kama Rigathi Gachagua ndiye alikuwa shida, ndio mlikuwa mnaweka ushuru ukuwe juu si mpunguze sasa vile ametoka?” Gachagua alisema.

Gachagua alibanduliwa ofisini mwezi uliopita baada ya kushtumiwa kwa jumla ya mashtaka 11 ambayo yaliwasilishwa bungeni na mbunge wa Kibwezi Magharibi, Mwengi Mutuse.

Baada ya kubanduliwa na seneti, aliyekuwa waziri wa masuala ya ndani, Kithure Kindiki aliapishwa wiki mbili baadae kama naibu rais mpya katika ukumbi wa KICC.

Kindiki aliapa kutomuangusha rais Ruto katika kuendesha serikali yake, akiahidi kufanya kazi sako kwa bako, bega kwa began a bosi wake katika kutimiza manifesto yake ya 2022.

Kuapishwa kwake kulikuwa kumechelewa baada ya mawakili wa Gachagua kuelekea mahakamani kupinga kubanduliwa kwake na bunge la seneti.