Rais mstaafu Uhuru Kenyatta amewashauri viongozi wa Kenya kuheshimu wananchi ili kupata heshima sawia.

Akihutubu katika kaunti ya Embu wakati wa kusimikwa kwa askofu Peter Ndung’u kusimamia jimbo la kanisa Katoliki Embu, Kenyatta alisema kwamba ili Kenya kupata maendeleo na kusonga mbele, inahitaji viongozi ambao watawaheshimu wananchi wake.

Aliwataka Wakenya wote kuungana na kuombea taifa, akisisitiza haja ya kukomeshwa kwa siasa za kikabila.

“Tuombee nchi yetu, tuombee Amani na uwiano kati ya viongozi na wananchi. Tuache mambo ya ukaabila na tupendane. Sisi wote ni Wakenya na Kenya haiwezi kufaulu watu wakiwa na utengano, wakiwa wanatupiana maneno bila kuheshimiana.”

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

“Viongozi heshimu wananchi na wao watarudisha hiyo heshima,” Kenyatta alisema.

Kiongozi huyo mstaafu alitania akisema kwamba yeye siku hizi hana maneno mengi bali husikiza redio na kutazama runinga tu.

“Unajua mimi siku hizi sina stori mingi, mimi huwa naangalia tu TV na kusikiliza redio,” aliongeza.

Rais mstaafu alimuahidi askofu mpya kwamba yeye wakati atamualika katika ibada ya kuchanga pesa kwa ujenzi wa kanisa, hatopeleka siasa kanisani bali lake litakuwa tu lile aliloitiwa.

“Nakuhakikishia mimi sitaleta siasa kanisani lakini nitakuja kwa yale tu uliyoniitia, kujenga kanisa la Mungu. Kwa hivyo wakati wowote, jisikie huru kutukaribisha,” Kenyatta alimaliza.

Mkutano huo wa kidini uliofanyika Jumamosi uliluwa wa kwanza kwa Rais Ruto kukutana ana kwa ana na aliyekuwa naibu wake Rigathi Gachagua ambaye alibanduliwa ofisini mwezi mmoja uliopita.

Ulikuwa ni mkutano ambao uliwakutanisha pia na rais mstaafu Uhuru Kenyatta katika eneo la Mlima Kenya kwa mara ya kwanza tangu alipochukua madaraka kutoka kwake mwezi Septremba 2022.

Hata hivyo, licha ya viongozi kupewa nafasi ya kuzungumza, Gachagua hakuweza kuzungumza.

Picha zake akitembea kwenye matope kuelekea kwenye ukumbi mkuu ziliizua mjadala mkuu kwenye mitandao ya kijamii ambapo aliketi mbali na viongozi wengine.