Aliyekuwa naibu rais, Rigathi Gachagua amewakosoa baadhi ya wandani wa rais Ruto kwa kile alisema ni kuwashambulia viongozi wa kanisa.

Akizungumza katika ibada ya kanisa huko Kajiado, Gachagua alisema kwamba alisikitishwa sana kuona makumi ya wandani wa Ruto wakiwashambulia maaskofu wa Katoliki baada ya kutoa taarifa ya kuikosoa serikali kwa utendaji wake mbaya.

Gachagua aliwashauri viongozi hao kuwaheshimu viongozi wa kanisa, akisema kwamba wao ndio wanajumuika na wananchi wa kawaida karibia kila siku.

DP huyo wa zamani alisema kuwa wanachosema viongozi wa makanisa kinafaa kutiliwa maanani kwani wao ndio wako na mwananchi wa kawaida muda wote.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

“Kama kuna viongozi wanaofanya public participation kila siku ni viongozi wa kidini kwa sababu wako na waumini kila siku, kila wikendi. Na kama kuna watu wanaojua chenye ground inasema, ni viongozi wetu wa kanisa. Kwa hivyo, ukisikia viongozi wetu wanasema kitu, tuwasikilize na tuwaheshimu,” Gachagua alisema.

“Tulisikitishwa sana wakati viongozi wetu wa kanisa Katoliki walipozungumza na tuliona baadhi ya wabunge wakiwatukana, wakiwazomea na kudharau baba zetu wa Imani.”

“Wale ni wapakwa mafuta wa Mungu, na ni sharti tuwaheshimu,” Gachagua aliongeza.

Kiongozi huyo wa zamani hata hivyo alimpongeza rais Ruto kwa kuzungumzia suala hilo Jumamosi katika ibada ya kusimikwa kwa padre Peter Ndung’u kama askofu mpya wa jimbo la Katoliki Embu.

“Na nina furaha kwamba jana rais wetu Dkt William Ruto alitambua kwamba maaskofu wa Katoliki waliibua masuala fulani na alisema kwamba watasikilishwa au kupewa nafasi ya kujieleza. Huo ndio mkondo salama wa kufuata.”

“Tungependa kuwaambia wale waheshimuwa wengine waliowatukana maaskofu wa Katoliki, achene kiburi,” Gachagua alisema.

Alhamisi wiki jana, baraza la maaskofu wa kanisa Katoliki nchini lilifanya mkutano na waandishi wa habari na kuituhumu serikali ya William Ruto katika kile walichosema kuwa ni utendakazi mbaya.

Maaskofu hao walimsuta Ruto wakidai kwamba uongozi wake umefanya kuwa kawaida itikadi za kudanganya pamoja na ongezeko la ufisadi nchini.

Walimtaka rais kusikiliza vilio vya mwananchi wa kawaida, wakisema kwamba idadi kubwa ya Wakenya hawajafurahishwa na uongozi wake, miaka 2 tangu alipochukua uongozi wa taifa.