Mbunge wa Mumias Mashariki, Peter Salasya amedai kuwa mswada wa fedha wa mwaka 2024 uliotupiliwa mbali na rais Ruto mnamo Julai umerejeshwa kisiri.

Akifichua haya kupitia ukurasa wake wa Facebook, Salasya alisema kwamba mswada huo licha ya kutupiliwa mbali, kuna njama ya kurudishwa na safari hii unaungwa mkono na ODM.

Salasya alisema wabunge wengi kutoka ukanda wa Mlima Kenya wameupinga lakini akatilia mashaka kwamba chama cha ODM ndicho kinaunga mkono kurejeshwa kwa mswada huo, akidai wameweka ahadi ya kutorekebisha hata kikomo.

“Mswada wa fedha wa 2024 uliotupiliwa mbali umerudi na nina furaha baadhi ya wanachama wa serikali ya Kenya Kwanza kutoka Mt Kenya wamekataa. Adui pekee wa Wakenya ni ODM wakiongozwa na kiongozi wao wa wengi anayesema kwamba hakuna koma inafaa kubadilishwa kwenye mswada wa fedha wa 2024,” Salasya alitoa kauli hiyo yenye ukakasi mwingi.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Adha, mbunge huyo alisisitiza kwamba Wakenya hawako tayari kwa mswada huo na wanasimama kidete kuonyesha hasira zao dhidi ya mswada huo uliotajwa kama kandamizi.

“Utakubali tena huu upuuzi mara hii ama? Tutakataa hata kabla haujarudi kwa siri ndani ya nyumba,” mbunge huyo alisema.

Itakumbukwa mswada wa fedha wa 2024 ulitupiliwa mbali na rais Ruto mnamo Julai baada ya msururu wa maandamano ya kuupinga ambayo yalidumu kwa wiki kadhaa.

Maandamano hayo ambayo yalianza mnamo Juni yalifikia kilele chake Juni 25 wakati kundi la mamia ya vijana walipovunja ua na kuingia katika majengo ya bunge kwa fujo mno.

Machafuko hayo yalishuhudiwa kwa siku kadhaa baadae, kupelekea rais Ruto kutupilia mbali mswada huo lakini pia kulivunja baraza lake la mawaziri.

Baadae aliteua baraza jipya ambalo lilijumuisha wanachama wa ODM, akiwemo John Mbadi ambaye alipewa wizara muhimu ya fedha.

Wiki iliyopita katika mahojiano kwenye runinga moja nchini, waziri Mbadi alisema kuwa upo mpango wa kutowasilisha mswada wa fedha wa 2025 bungeni mwaka ujao.