Mbunge wa Laikipia Mashariki, Mwangi Kiunjuri, amemkosoa vikali Kiongozi wa DCP, Rigathi Gachagua, kwa kuwadhalilisha yeye pamoja na Mbunge mwenzake, Kimani Ichung’wah, kwa madai ya kuwa maadui wa jamii ya Wakikuyu.
Mapema siku hiyo, Gachagua aliwatuhumu wawili hao kwa kushirikiana na serikali ya Kenya Kwanza kwa njia zinazokiuka maslahi ya jamii yao, jambo lililomfanya Kiunjuri kujibu kwa ukali.
Gachagua, ambaye ni Makamu wa Rais wa zamani, alitoa matamshi hayo yenye utata alipokuwa akihutubia Wakenya waishio ughaibuni nchini Marekani siku ya Jumatatu.
Hata hivyo, kupitia taarifa aliyoitoa saa chache baadaye, Kiunjuri alitaja kauli hiyo ya Gachagua kuwa ya uongo, ya kashfa na ya uchochezi, akidai inalenga kuigawanya jamii ya Wakikuyu na kuleta migawanyiko ya vurugu.
“Rigathi atashuka hadi kiwango gani? Napinga vikali matamshi haya yasiyo na msingi, ya kashfa na uchochezi ambayo yanalenga kuchochea chuki, vurugu, vitisho na ghasia dhidi ya wale anaowataja kuwa maadui wake, na kwa upana zaidi, maadui wa watu,” alisema Kiunjuri.
“Wakenya wanapaswa kumtambua Rigathi alivyo—kiongozi wa kiimla, asiye na staha, matusi na vitisho vikimtawala, ambaye hawezi kuvumilia maoni tofauti,” aliongeza.
Alimwelezea Gachagua kama dikteta asiyevumilivu anayewahukumu wapinzani wa kisiasa na kuhimiza chuki dhidi yao, akimlaumu kwa kukosa ajenda yoyote ya maendeleo.
“Hakawii kugeuza maoni tofauti kuwa uhalifu, hata hadi kufikia hatua ya kutaka wanaomkosoa waadhibiwe. Siasa zake zinaelekea kwenye vurugu hatari, na lazima awajibishwe,” alisema.
“Ni jambo la kusikitisha kuwa mtu anayejinadi kuwa kiongozi wa Mlima Kenya hana ajenda yoyote zaidi ya kuchochea, kugeuza tofauti kuwa kosa, na kupiga porojo zisizo na maana.”
Kiunjuri alikumbusha tukio ambapo Gachagua aliwachochea watu wa Mlima Kenya dhidi ya wanamuziki waliomuunga mkono Naibu Rais, Kithure Kindiki, hali iliyowafanya baadhi yao kunyanyaswa.

Alisema kuwa matumizi ya vurugu ni siasa za zamani zisizokuwa na nafasi tena nchini Kenya, na kuhimiza siasa za hoja badala ya vitisho.
“Ninawaomba Wakenya waliosikiliza hotuba hiyo pamoja na wengine kwa jumla wazingatie ni mara ngapi Gachagua amezungumza kuhusu maendeleo au changamoto zinazokumba eneo hili ama taifa,” alisema.
“Amekuwa akijawa na chuki na kila mara anatafuta kulipiza kisasi kisiasa kwa nguvu. Namkumbusha kuwa ghasia ni siasa zilizopitwa na wakati, na hazina nafasi katika taifa letu.”
Kiunjuri aliwataka wapiga kura wake watambue aina ya uongozi wa kugawa watu na kutetea ushindani wa kisiasa unaojengwa kwenye hoja, si chuki.
“Anaonekana kuwa na nia ya kuipeleka Kenya katika machafuko. Hatutaruhusu. Mimi nitasimama kidete na sitakubali kutishwa na Rigathi. Tofauti za kisiasa zipo, lakini hazipaswi kuchanganywa na chuki, uchochezi na vitisho,” alisema.
Aliwakumbusha wananchi kuhusu historia ya Gachagua ya kutumia vitisho, akisema tabia hiyo ni hatari kwa mshikamano na maendeleo ya jamii ya Wakikuyu.
“Si muda mrefu uliopita, aliwachochea watu wa Mlima Kenya dhidi ya wanamuziki aliowaona kama wasaliti kwa kuhudhuria hafla ya Naibu Rais Kithure Kindiki,” alisema.
“Matokeo yake yalikuwa ni unyanyasaji wa baadhi ya wanamuziki hao. Je, Rigathi ndiye mlinzi wa maamuzi binafsi na ya kijamii ya watu wa Mlima Kenya? Je, ataacha nini ili apate mamlaka na umaarufu wa kupangwa katika eneo hili?” alihoji.
“Nawaomba watu wetu waepuke kiongozi anayelekeza jamii yetu katika kutengwa kwa kueneza chuki zisizoisha dhidi ya wale wanaoamua kushirikiana na jamii nyingine nchini Kenya,” alisema.
Alimtaka Gachagua kuruhusu ushindani wa hoja kuendelea na kuacha kusambaza uongo na chuki dhidi yake na viongozi wengine.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!