Afisa wa polisi anayeaminika kuwa na matatizo ya afya ya akili alifyatua risasi na kumuua mwenzake katika Kituo cha Polisi cha Ng’iya, Kaunti ya Siaya, mapema Jumapili asubuhi.

Mamlaka zinaamini kuwa tukio hilo huenda lilichochewa na mzozo wa kibinafsi au hali ya matatizo ya afya ya akili.

Tukio hilo lilitokea majira ya saa 12:00 asubuhi wakati Konstebo Martin Mwendwa anaripotiwa kumpiga risasi na kumuua afisa wake wa juu, Koplo Chesise, ambaye alikuwa mkuu wa kituo hicho.

Kwa mujibu wa polisi, Mwendwa alijizatiti kwa bunduki aina ya G3, akaingia katika makazi ya koplo huyo na kufyatua risasi — na kumpiga kwa risasi kifuani na mikononi hadi kufa.

Akithibitisha tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Gem Yala, Charles Wafula, alisema maafisa waliokuwa katika kituo hicho waliitikia kwa haraka mara baada ya risasi za kwanza kusikika.

Konstebo Mwendwa alijaribu kukimbilia Shule ya Upili ya Wasichana ya Ng’iya, lakini alikabiliwa na kuuawa kwa kupigwa risasi na maafisa wenzake wakati wa makabiliano.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Ingawa uchunguzi wa awali unaashiria uwezekano wa mzozo wa kibinafsi kati ya maafisa hao wawili, polisi pia wanachunguza uwezekano kuwa Mwendwa alikuwa anapitia hali ya kiakili wakati wa shambulizi hilo.

“Swala hili linachunguzwa, na tunalenga kubaini chanzo halisi. Hatufungi mlango kwa uwezekano wowote, ikiwa ni pamoja na msongo wa akili,” alisema Bw. Wafula.

Miili ya maafisa hao wawili imepelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Siaya kwa uchunguzi wa kitabibu huku uchunguzi ukiendelea kubaini kiini cha makabiliano hayo ya kufa mtu.