
NAIBU wa rais profesa Kithure Kindiki amesisitiza kwamba ziara ya rais William Ruto katika ukanda wa Mlima Kenya kuanzia wiki ijayo haitakuwa ya kisiasa.
Akizungumza katika kaunti ya Murang’a Alhamisi, Kindiki aliweka wazi kwamba ziara hiyo ya wiki moja ya rais Ruto Mlimani itakuwa tu ya kuzindua miradi iliyokamilika na mingine itakayoanza kutekelezwa.
Kulingana na Kindiki, Ruto atakuwa akizindua masoko yaliyojengwa na serikali na kuyakabidhi kwa wafanyibiashara, ujenzi wa barabara miongoni mwa miradi mingine.
“Wiki ijayo, Mungu akipenda, Rais atazuru Murang’a, na hautakuwa mkusanyiko wa kisiasa. Anakuja kufungua rasmi masoko yetu yaliyokamilika, kushughulikia masuala ya umeme, kuboresha barabara zetu, na kukagua miradi inayoendelea ya unyunyizaji maji mashambani hapa," Kindiki alisema.
Akionekana kumlenga mtangulizi wake aliyebanduliwa Oktoba mwaka jana, Kindiki alisema kwamba huu si wakati wa kupiga debe za kisiasa bali ni wakati wa kufanyia wananchi kazi.
Kindiki alifafanua zaidi kwamba kufanya siasa si jukumu la serikali bali ni jukumu la upinzani.
"Jukumu la serikali sio kutanguliza siasa. Hiyo ni kazi ya upinzani. Wajibu wa serikali ni kuhakikisha kwamba miradi ya wananchi inafuatiliwa haraka na kutolewa," aliongeza.
Ruto anatarajiwa kuanza ziara yake rasmi ya kwanza katika eneo la Mlima Kenya tangu kung’atuliwa ofisini kwa aliyekuwa Naibu Rais, Rigathi Gachagua, ambaye kwa muda mrefu amejifanya kuwa kinara wa kisiasa wa eneo hilo.
Tangu kutimuliwa kwa Gachagua, eneo la Mlima Kenya limekuwa na mgawanyiko mkubwa, huku mrengo mkubwa ambao hapo awali ukimuunga mkono Ruto kutokana na Gachagua sasa kuhama utiifu wao kwingine.
Mnamo Alhamisi, Machi 20, 2025, Mbunge wa Gatanga Edward Muriu alionya rais dhidi ya kutaja jina la Gachagua au mapatano yake ya kisiasa na Raila Odinga katika ziara yake ijayo ya eneo la Mlima Kenya.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!