
MBUNGE wa Gatundu Kusini, Gabriel Kagombe ametoa wito kwa serikali kumpa aliyekuwa mwenyekiti wa tume ya uchaguzi na mipaka IEBC, Wafula Chebukati mazishi ya kitaifa kama shujaa.
Akizungumza Jumamosi, Kagombe alisema kwamba Chebukati alisimama tisti kwa ujasiri kuhakikisha kwamba taifa la Kenya halikutumbukia katika machafuko ya baada ya uchaguzi wa Agosti 2022, hivyo anastahili heshima zote za kishujaa katika mazishi yake.
“Tutamkumbuka Chebukati kwa kuwa mtu mkakamavu, mtu shupavu, mtu ambaye alipigania haki ya Wakenya, mtu ambaye hakuogopa hata alipopewa vitisho vya woga alisimama kidete na kusema kwamba haki ya Wakenya lazima ipatikane,” Kagombe alitoa risala zake za rambirambi kwa marehemu Chebukati.
“Mimi nataka kumkumbuka kwamba mwaka 2022 tulikuwa katika hali mbaya ambapo nchi hii ingepasuka, vita vingetokea. Na tunaona ya kwamba yeye alisimama kidete na kusema ukweli, yale ambayo yalileta vita 2007 ni kwa sababu yule aliyekuwepo hakusimama kidete, lakini Chebukati alisimama na kusema ukweli.”
“Mimi nasema kwamba Chebukati ni shujaa ambaye anastahili kupatiwa heshima yake na mimi najua hata nchi hii na serikali itampa mazishi ama buriani ya kufaa,” Kagombe alijieleza.
Wafula Chebukati aliteuliwa kuwa mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) na Rais wa wakati huo Uhuru Kenyatta Januari 2017.
Alisimamia uchaguzi mkuu wa 2017 na 2022, ambapo alikabiliwa na changamoto kadhaa kabla ya kustaafu 2023.
Matokeo ya uchaguzi wa urais wa 2017 yalibatilishwa na Mahakama ya Juu kwa sababu ya kasoro zilizobainishwa, na hivyo kuwa mara ya kwanza kwa uchaguzi wa urais kubatilishwa nchini Kenya. Hata hivyo, Chebukati aliongoza tume hiyo kupitia uchaguzi wa marudio uliofuata.
Katika uchaguzi wa 2022, Chebukati alimtangaza William Ruto kuwa Rais mteule licha ya migawanyiko ndani ya tume hiyo ambayo ilizua taharuki kwa umma.
Alisimama kidete na matokeo yaliyotangazwa, ambayo hatimaye yaliidhinishwa na Mahakama ya Juu.
Alipostaafu mnamo Januari 2023, Chebukati alituzwa Mzee wa Agizo la Moyo wa Dhahabu (EGH), heshima ya pili ya juu ya kiraia nchini Kenya, kwa kutambua utumishi wake.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!