Operesheni ya Polisi Isiolo, kaunti za Marsabt

Takriban bunduki kumi za aina mbalimbali zimepatikana katika Operesheni "Ondoa Jangili" inayoendelea katika Kaunti za Isiolo na Marsabit.

Operesheni hiyo ilianzishwa mnamo Februari 3, 2025 ikilenga makundi ya uhalifu yanayoendeshwa na waliosalia kutoka kwa Jeshi la Ukombozi la Oromo (OLA) katika kaunti hizo mbili.

Msemaji wa polisi Michael Muchiri alisema Jumamosi, Februari 22 jumla ya kambi 14 za muda, zinazoaminika kuanzishwa na wahalifu hao, zimeharibiwa.

"Miongoni mwa marejesho yaliyopatikana ni pamoja na, silaha na risasi 10 za aina mbalimbali, mabegi ya bunduki, fedha feki za Dola za Marekani na Ethiopian Birr, lori la maji, pikipiki 9, magari mawili, gunia lililojaa bangi yenye uzito wa takriban kilo 200, vyakula, paneli za jua, seti ya vifaa vingine vya kijeshi," alisema.

Kutokana na operesheni hiyo inayoendelea, shughuli kama vile kuzagaa kwa silaha ndogo ndogo, uchimbaji haramu wa madini, biashara haramu ya binadamu, uvamizi wa mipakani na utekaji nyara ili kujipatia fedha, zimepunguzwa.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

"Hii imemaliza mateso yasiyoelezeka yanayowapata watu wanaoishi kwenye mpaka wa Kenya na Ethiopia."

Polisi walisema kundi hilo limechukua fursa ya uhusiano wa karibu wa kifamilia na kitamaduni kati ya Waborana wa Kenya na Oromo ya Ethiopia kujipenyeza na kujificha miongoni mwa watu na kuendelea kufanya ukatili na kusababisha mateso yasiyoelezeka.

Aliongeza wataendelea na zoezi la kutuliza eneo hilo.

Operesheni hiyo ilikuja baada ya Rais William Ruto mnamo Januari 2025, kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Huduma ya Usalama ya Kitaifa ya Ujasusi wa Ethiopia, Redwan Hussien akishirikiana na Mkurugenzi Mkuu wa Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi ya Kenya Noordin Haji.

Mkutano huo ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi na inasemekana suala hilo lilihusika katika shughuli hiyo.

OLA ni kundi la upinzani lenye silaha linalofanya kazi katika Mkoa wa Oromia nchini Ethiopia.

OLA inahusisha zaidi wanachama wa zamani wenye silaha wa mkataba wa kabla ya amani na Oromo Liberation Front (OLF) ambao walikataa kupokonya silaha kwa kutilia shaka mpango huo, na waandamanaji wa zamani wa vijana ambao walikua wamekatishwa tamaa na upinzani usio na vurugu.

Mkuu wa polisi Douglas Kanja alisema operesheni hiyo ya kiwango cha juu itawalenga wahalifu wanaoendesha oparesheni haramu ambazo zinatishia usalama wa taifa la Kenya.

"Hizi ni pamoja na silaha, ulanguzi wa dawa za kulevya na ulanguzi wa binadamu, uchimbaji madini haramu, kuchochea migogoro ya kikabila na utekaji nyara ili kupata fidia haswa katika Kaunti Ndogo za Sololo, Moyale, North Horr, na Merti," alisema.

Aliwahakikishia wanajamii katika maeneo yaliyotajwa hapo juu usalama wao huku pia akiwasihi kuwa watulivu na kushirikiana na timu za usalama mashinani.

Polisi wanataka wenyeji katika maeneo haya kuwa watulivu na kushirikiana kikamilifu na vyombo vya kutekeleza sheria kwa kupeana taarifa muhimu kwa mafanikio ya operesheni hii ya wakala mbalimbali.