KATIBU katika wizara ya usalama wa ndani Raymond Omollo amefichua kwamba maafisa wa polisi wa Kenya waliotumwa nchini Haiti wamepiga hatua kubwa katika kurudisha amani na utulivu mitaani katika jiji la Port-au-Prince.


Omollo alitoa taarifa hizo kupitia ukurasa wake kwenye X alipochapisha klipu ya afisa mmoja wa Kenya akiwaimbisha watoto darasani nyimbo za Kiswahili na tafsiri kwa Kifaransa.


Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Omollo alisema kwamba kabla ya maafisa wa polisi wa Kenya kupelekwa nchini Haiti, mitaani kulikuwa na machafuko ambayo yalifanya shughuli za masomo kuwa ngumu.


Wahalifu waliwachukua watoto na kuwatumia kama vichocheo kwenye vita ambavyo vilizua taharuki kimataifa.


“Polisi wa Kenya, wanaoongoza ujumbe wa kulinda amani unaoungwa mkono na Umoja wa Mataifa nchini Haiti, wamepata maendeleo ya ajabu katika kurejesha utulivu, hasa katika sekta ya elimu.”


“Kwa miaka mingi, unyanyasaji wa magenge ulikumba jamii, huku watoto wa umri wa kwenda shule mara nyingi wakiandikishwa kama vichocheo katika migogoro hii, na kuwanyima elimu na hali ya kawaida,” Omollo alichapisha.


Omollo alisisitiza kuwa mafanikio ya misheni hiyo yanawakilisha hatua muhimu ya kuvunja mzunguko wa vurugu na kutoa matumaini kwa vijana wa Haiti.


"Shule zimefunguliwa tena, na watoto ambao hapo awali walinaswa katika vita vya magenge sasa wamerudi madarasani, wakidai tena haki yao ya elimu na mustakabali mwema.


 


"Hatua hii muhimu inasisitiza mafanikio ya ujumbe wa kulinda amani katika kuvunja mzunguko wa vurugu na kuendeleza matumaini kwa vijana wa Haiti, kuhakikisha kuwa wameandaliwa kujenga taifa lao," Omollo aliongeza.


Taarifa hii inafuatia kutumwa hivi majuzi kwa maafisa 217 zaidi wa polisi wa Kenya nchini Haiti mnamo Ijumaa, Januari 17, 2025.


Katibu wa Baraza la Mawaziri Kipchumba Murkomen, PS Omollo, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja, na maafisa wengine wakuu walisimamia kutumwa.