MWINJILISTI mkongwe wa humu nchini, Reuben Kigame amesifia hatua ya ujasiri ya mwanaharakati Okiya Omtatah ya kutangaza kuwa atawania urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

Kupitia ukurasa wake wa X, Kigame alisema kwamba Omtatah ni mmoja kati ya watu ambao amekuwa akifurahia kazi zao katika harakati za kutafuta haki kortini na kwamba hatua yake ya kujitosa kwenye kinyang’anyiro cha urais ni jambo la kushabikiwa.

“Heri ya kuzaliwa Comrade @OkiyaOmtatah. Wewe ni pumzi ya hewa safi na Kenya imebarikiwa kuwa na wewe hai kwa wakati huu. Wewe ni mshindani anayestahili katika kinyang'anyiro cha urais ujao,” Kigame aliandika akimtakia heri njema ya kuzaliwa mwanaharakati huyo.


Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans


Hata hivyo, Kigame aliweka hisia zake wazi kuhusu hatua ya Omtatah kuwania urais, akimshauri kuungana naye ikiwa kweli ana nia ya dhati ya kuirudisha Kenya katika kile alichokitaja kuwa ni ‘mkondo stahiki.’

Alimrai Omtatah kuiasa timu yake kutathmini uwezekano wa kufanya kazi na timu yake ili kupata njia mwafaka ya kuikomboa nchi kutoka utawala wa rais wa sasa William Ruto, ambao anahisi umewafeli Wakenya katika ahadi nyingi za wakati wa kampeni.

“Natumai timu yako ya tathmini ya rais itakuwa na unyenyekevu wa kuketi na timu yangu ya rais ili kuunda mkakati mzuri wa kushirikiana. Usisahau kamwe, haikuhusu wewe au Kigame, lakini njia bora zaidi ya kuokoa nchi yetu kutokana na uharibifu zaidi, kurejesha maadili na kuweka viongozi wanaoongozwa na tabia, kumaliza wala rushwa, na kupata maisha ya baadaye ya watoto wetu,” Kigame alisema.

Alimaliza kwa kumtakia Omtatah maisha marefu na kuishi hadi pale atakapotimiza ndoto yake ya kubadilisha Kenya kisiasa.



“Uishi kuona siku nyingi zaidi za kuzaliwa na Mola akatujalia kuunda serikali ijayo pamoja na wewe au Kigame kama rais ajaye.”

Kigame anamwandikia Omtatah ujumbe hii ikiwa pia naye analenga kiti hicho cha urais.

Ikumbukwe Kigame alikuwa miongoni mwa wale waliotaka kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2022 lakini hakufanikiwa kufika debeni baada ya tume ya uchaguzi na mipaka, IEBC kumfungia nje kwa kutokuwa na stakabadhi husika.

Kigame alihamia mahakamani kupinga hatua ya IEBC kumtupa nje lakini kesi yake ilijikokota hadi baada ya kumalizika kwa uchaguzi huo.