MSHAURI wa masuala ya kiuchumi wa rais William Ruto, Moses Kuria amewaasa wananchi kujiunga na mpango wa bima ya matiba ya SHA hata kama hawampendi rais William Ruto.

Akizungumza katika eneobunge la Manyatta kaunti ya Embu, Kuria aliwataka wananchi kufunguka macho na kutohadaiwa kwamba mpango wa Taifa Care hauwafai.

Kwa mujibu wa Kuria, baadhi ya viongozi wanaowataka Wakenya kutojisajili katika mpango wa SHA wana bima zao za nguvu za matibabu na hawatokuwa nao hospitalini wakati watakuwa wanataabika kutafuta matibabu bila bima ya SHA.

Akitolea mfano, Kuria alisema kwamba mwananchi wa kawaida kuambiwa na kiongozi kutojisajili SHA ni sawa na kunywa sumu na kutarajia Kuria afariki.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans



“Huu mpango ni wako, si wa serikali, si wa Kuria wala rais Rut. Ni wako! Siku utagonjeka ukiwa hospitalini utaanza kusema ni Ruto? Unajua mimi naona watu wengine wakileta mchezo katika hili suala, ni kama kunywa sumu ukitarajia Moses Kuria afe, na wewe ndiye umekunywa sumu. Nikakufaje na sumu ambayo wewe umekunywa?” Kuria alihoji.

“Hivyo wakati mtu anakuambia kutojisajili kwa Taifa Care, siku ya kugonjeka mktakuwa na yeye kwenye wodi? Mtakuwa na yeye hospitalini? Wakati unafanya harambee ya kupata pesa za matibabu sababu mtu wako amelazwa, mtakuwa na yeye? Kwa hivyo tujichunge dhidi ya uongo jamani,” aliuliza zaidi.

Aliwataka wale wanaomchukia rais William Ruto kutambua kwamba wanacheza karata tata na afya zao kwa kukataa kujisajili kwenye SHA kisa hawampendi rais.

“Na hata kama humtaki rais, si uingie katika hii SHA, ndio utibiwe, ndio uishi miaka mingi ya kumtukana. Ukianza kumtukana na hujajisajili, utaishi miaka mingi kweli ya kumtukana? Si angalau utibiwe ndio uweze kumtukana kesho jamani! Kwa sababu huu mpango ni wako,” Kuria aliwaambia wananchi.



Mshauri huyo wa rais alisema kwamba wengi wanalalamika kuhusu mapungufu ya SHA bila kutambua kwamba ina miezi miwili tu tangu izinduliwe.

Aliwataka Wakenya kuwa wenda pole katika kunyoosha vidole vya lawama kwa mpango huo kwani ndio mwanzo uko katika hatua za mwanzo mwanzo na kwamba utaboreshwa zaidi kadri siku zinazidi kusonga.

“Bado zimesalia siku chache kabla ya SHA kuadhimisha miezi miwili. Sasa huyu mtoto wa miezi 2 ndiye mnataka aanze kucheza raga jamani? Inawezekana kweli? Najua watu wengi watakukatisha tamaa, lakini kadri wanavyokukatisha tamaa wakumbushe kwamba ni miezi miwili tu, hata hatujaanza kufunga Kamba za viatu, na sasa ndio tunaanza,” Kuria alitetea SHA.



Mpango wa SHA ulianza rasmi kufanya kazi mnamo Oktoba mosi lakini umepokelewa na Wakenya kwa hisia vuguvugu, wengi wakionekana kuukosoa mpango huo kwa kutokuwa sahihi katika matibabu yao.

Wiki jana katika hotuba yake kwa nchi katika kikao cha pamoja cha mabunge yote mawili, rais Ruto aliutetea mpango huo akiwataka wale wanaolalamika kuhusu mapungufu yake bila kujisajili kufanya hatua ya kujisajili kwanza kabla ya kuanza kuibua maswali kuhusu matatizo ya SHA.