
MWANAHARAKATI Morara Kebaso amemuomba Mungu
kudhihirisha wazi uwepo wake katika azma yake ya kuwania urais wa Kenya katika
uchaguzi mkuu ujao wa 2027.
Kupitia ukurasa wake wa X, Kebaso alimtaka Mungu
kumuonyesha ishara kama kweli ni yeye anataka awanie urais, ili isije kuonekana
kama ni mwenyewe anataka au pengine anafanya kazi ya bure.
“Bwana.
Ikiwa ni wewe unayenituma, nipe ishara. Sitaki kufanya hivi kwa matamanio yangu
au hamu yangu. Nionyeshe ishara ikiwa wewe ndiye unayenituma. Nataka kujua kama
ni wewe unayezungumza name,” Kebaso alisema.
Ombi la Morara linajiri siku chache baada ya kutangaza
rasmi kuwa atakuwa debeni katika uchaguzi wa urais mwaka 2027.
Mwanzilishi huyo wa chama cha INJECT alisema kuwa
bila wasiwasi wowote, atakuwa miongoni mwa wale watakaomenyana na rais Ruto
katika kinyang’anyiro cha urais mwaka 2027.
Hii ni licha ya kusutwa na wengi kwamba hana pesa za
kumwezesha kufanikisha kampeni za urais ambazo humu nchini hushuhudia wagombea
wakizunguka nchi nzima katika kipindi cha takribani miezi 4 ya kampeni.
Hata hivyo, Kebaso alikiri kwamba ni kweli yeye ni
omba omba lakini akasema si kupenda kwake kuwa hivyo.
Mwanaharakati huyo alisema yeye, sawa tu na Wakenya
wengine wengi, wameshrutishwa kuwa ombaomba na uongozi wa serikali ya rais Ruto
ambayo anaituhumu kwa kufanya mazingira ya kiuchumi kuwa mabaya.
“Ndio
sisi ni ombaomba. Lakini hatufurahii kuomba. Inashusha utu wetu. Ikiwa
tungekuwa na pesa za kutosha, tungeendesha kampeni ya elimu ya uraia bila
kuombaomba.”
“Vijana
wengi nchini Kenya wamefanywa kuwa ombaomba kama sisi. Wanaomba kazi. Wanaomba
kupandishwa vyeo. Wanaomba mtaji. Wanaomba chakula. Wanaomba takrima. Wanaomba
jamaa zao. Wanaomba marafiki zao. Wanaomba wanasiasa. Ni wakati wa ombaomba
kurudisha nchi yao. Kujitengenezea ajira na fursa. Kuwajengea wazazi nyumba na
kuwalisha wadogo zao. Tunataka nchi yetu irudi,”
Kebaso alisema katika tweet nyingine.
Licha ya kuweka wazi kwamba atakuwa debeni,
mwanaharakati huyo alidokeza kuwa huenda akashirikiana na mwanaharakati mwenza,
Okiya Omtatah katika kuendesha kampeni za kutwaa urais 2027.
Alisema hayo baada ya Omtatah naye kutangaza kuwa
tayari ameanzisha mchakato mzima wa kutathmini hali itakayomuona akiwa debeni
katika kinyang’anyiro cha urais 2027.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!