Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

MWANAHARAKATI wa elimu ya kiraia, Morara Kebaso amedokeza uwezekano wa kufanya kazi pamoja na mwanaharakati wa haki za kibinadamu Okiya Omtatah kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Kupitia ukurasa wake wa X, Kebaso alifichua kwamba amaheshimu sana seneta huyo wa Busia katika kile ambacho amefanya si tu katika siasa za Kenya lakini pia katika kutafuta haki kiuharakati mahakamani.

Kebaso alisema kwamba huenda wakaungana pamoja katika siku zijazo ili kutoa mwongozo mpya wa siasa za Kenya, na haswa katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

“Okiya Omtatah ni mtu mahiri mwenye hekima kubwa na uadilifu. Ndani yake naona maadili ya pamoja. Niko tayari kufanya kazi naye siku moja katika siku zijazo,” Morara Kebaso alisema.

Kauli ya Kebaso inajiri siku chache baada ya Omtatah kudokeza kuwa huenda akajitosa kwenye kinyang’anyiro cha urais mwaka 2027.

Omtatah alisema kwamba tayari ameanzisha timu ya kutathmini uwezekano na mazingira yote ambayo yatamwezesha kujitosa katika uwanja huo mpana kumenyana na wanasiasa wengine wakongwe, akiwemo rais wa sasa, William Ruto ambaye atalenga kutetea nafasi yake kwa muhula wa pili.

Akitangaza azma hilo mwishoni mwa juma lililopita, Omtatah alifichua kuanzisha timu ya watu 6 ambao watafanya kazi kwa bidii za mchwa kutathmini hakli nzima ya kumwezesha kuwania urais.

"Tuko katika wakati muhimu katika historia ya taifa letu, na wito wa kuhudumu haujawahi kuwa wa dharura zaidi. Baada ya kutafakari kwa kina na kushauriana na washauri wanaoaminika, viongozi wa jamii, na wananchi kutoka tabaka mbalimbali, nina furaha kutangaza kuundwa kwa Kamati ya kutathmini Urais,” alisema Omtatah Saturday. 

Alisema kuundwa kwa timu hiyo ni "hatua muhimu katika kuhakikisha kwamba maono yetu ya siku zijazo yanawiana na matumaini na matarajio ya Wakenya."

Kamati hiyo itakayoongozwa na Mary Kathomi Riungu, itakuwa ofisini kwa muda usiozidi miezi 18 na itavunjwa mara tu seneta huyo atakapotangaza rasmi kuwania au uamuzi wake wa kutogombea.

Charles Ile Kabaiku atakuwa naibu mwenyekiti huku David John Bwakali akiwa mwanamikakati wa kisiasa na mashinani.

Omatata ni seneta wa mara ya kwanza na mwanaharakati anayejulikana kwa uhodari wake wa kuwasilisha kesi mahakamani kwa maslahi ya umma, haswa dhidi ya sera za serikali anazoziona kuwa za uonevu na zisizo halali. Alijiunga na siasa mnamo 2022 kama mgombeaji huru.

Tangazo hilo lilifuatia lile la Mwanaharakati Kebaso aliyetangaza mwanzoni wa juma lililopita kwamba atakuwa debeni katika uchaguzi wa urais 2027.

Kebaso alisema kwamba chama chake kipya cha INJECT kitatoa wawaniaji wa nyadhifa mbalimbali kote nchini.

Wengine ambao wanatarajiwa kuwania urais ni pamoja na Kalonzo Musyoka, Eugene Wamalwa, Jimmy Wanjigi miongoni mwa wengine.