GAVANA wa kaunti ya Trans Nzoia, George Natembeya amefichua kwamba kibarua chake kijacho ni kuwania urais wa Kenya.

Akizungumza katika ofisini yake, gavana huyo wa DAP-K aliweka wazi kwamba pindi atakapokamilisha hatamu yake kama gavana wa Trans Nzoia, ataelekeza macho na nguvu zote katika wadhifa wa urais.

Alichukua nafasi hiyo kuwashukuru watu wa Trans Nzoia kwa kumpa nafasi kuwaongoza kama gavana wao, akisema kwamba baada ya hapo, atajikita katika siasa za kitaifa.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Natembeya alisema kuwa hayuko tayari kuwania kama naibu rais wa mwaniaji yeyote, katika kile anaelewa kuwa naibu rais hana usemi mkubwa katika kupitisha baadhi ya sera.

“Kitu chochote katika siasa kinawezekana. Lakini kutoka pahali ninapokaa, baada ya kumalizana na hii kazi ambayo watu wa Trans Nzoia wamenipa, na ninashukuru kwa kweli watu kwa kunipa heshima na upendeleo wa kuwahudumia, nitaenda kukita macho yangu kwa ukakamavu kwenye urais,” Natembeya alisema.

“Pindi nitakapomalizana na ugavana, sitaki kwenda kuwa naibu. Kwa sababu huwezi badilisha vitu wakati wewe ni naibu. Nafasi yao ya kupenyeza huwa ni finyu, wakati mwingine hata kupeana ushauri mdogo unaweza kupelekea kubanduliwa. Hivyo hatutaki hivyo na Wakenya hafikiri wanataka mabadiliko kamili,” aliongeza.

Kamishna huyo wa zamani wa mkoa wa Bonde la Ufa alisema kwamba ili kuleta mabadiliko hayo ambayo watu wanataka, ni sharti asimame kama rais na si naibu wa mtu yeyote.

Alitumia fursa hiyo kuzungumzia maazimio yake ambayo angependa kuyaleta katika mabadiliko anayokusudia.

“Ninataka kujenga nchi ambapo wakati unaona talanta unaikuza badala ya kuiua. Lakini hapa Kenya kuna wanasiasa ambao baada ya kuona talanta, kitu cha kwanza kufanya ni kuiua. Tunataka kuwa na nchi ambayo sisi wote tunajisikia kuwa sawa,” alisema.

Gavana huyo alisema kwamba anashukuru sana kwa wale ambao wanapendekeza yeye kusimama kama rais wa Kenya wakati mmoja.

Tamko lake linajiri siku chache baada ya watu kadhaa kuweka wazi kuwa watawania urais katika uchaguzi wa 2027.

Wiki jana, wanaharakati Morara Kebaso na Okiya Omtatah walitangaza kila mmoja kuwa watawania urais katika uchaguzi wa mwaka 2027.

Wawili hao watamenyana na rais William Ruto ambaye atakuwa anatetea wadhifa wake kwa muhula wa pili lakini pia Eugene Wamalwa wa DAP-K ambaye mapema mwezi Novemba alitangaza kupewa Baraka na chama hicho kuwania urais.