
Rais William Ruto ameagiza idara husika katika wizara
za barabara na miundombinu na ile ya kawi kusitisha mara moja utoaji wa zabuni kwa kampuni tata ya Adani.
Akizungumza wakati akitoa hotuba ya hali ya taifa kwa
wananchi katika kikao cha pamoja cha wabunge na maseneta alasiri ya Alhamisi,
Ruto aliagiza kusitishwa mara moja kwa michakato ya utoaji wa kandarasi kwa
Adani.
Adani ilikuwa inalenga kupewa zabuni ya kusimamia
uendeshaji wa uwanja wa ndege JKIA kwa miongo 3 pamoja pia na kampuni ya
kusambaza umeme ya KETRACO.
“Sasa
naelekeza katika kuendeleza misingi iliyoainishwa katika ibara ya 10 ya katiba
ya uwazi na uwajibikaji na ya msingi kuhusu taarifa mpya zinazotolewa na vyombo
vya uchunguzi na mataifa washirika, kwamba wakala wa ununuzi ndani ya wizara ya
uchukuzi na wizara ya nishati na petroli mara moja kufuta mchakato unaoendelea
wa ununuzi wa upanuzi wa JKIA,” rais Ruto alisema.
Ruto alisema kwamba agizo hili ni kutokana na habari
ambazo serikali imepokea kutoka kwa mataifa marafiki kuhusu wasifu wa Adani.
Kiongozi wa taifa pia alitaka kuvunjwa mara moja kwa
mkataba uliotiwa saini hivi majuzi kati ya kampuni ya kusambaza umeme ya
KETRACO na Adani.
“Nimeagiza
mara moja kufutwa kwa mchakato unaoendelea wa ununuzi wa upanuzi wa JKIA na pia
mkataba uliokamilika hivi majuzi wa KETRACO,”
alisema
Kughairiwa huko kulikuja baada ya ripoti kuashiria kuwa mmiliki wa Adani Group na wakurugenzi wake wameshtakiwa nchini Marekani kwa madai ya udanganyifu.
Msemaji wa Kundi la Adani hata hivyo alikanusha makosa yoyote kwa upande wa wakurugenzi na mmiliki akisema kushtakiwa haimaanishi kuwa wana hatia.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!