
SENETA wa kuteuliwa, Karen Nyamu amemtaja marehemu Papa Francis kama mtu ambaye wengi wataukosa uwepo wake si tu katika uongozi wa kanisa Katoliki duniani bali pia katika ushauri na wosia wake kuhusu masuala mbalimbali ya kijamii.
Akizungumza kwenye runinga ya TV47 asubuhi ya Alhamisi, Nyamu alisema kwamba alivutiwa sana na jinsi Papa Francis alikuwa amejibeba katika maisha ya kawaida bila kujali tabaka lake.
Kwa mujibu wa Nyamu, Papa Francis alikuwa ni mtu ambaye alikumbatia waziwazi utandawazi na mitandao ya kijamii japo pia alionya kuhusu teknolojia ya AI na madhara yake.
“Nilimpenda Papa Francis kwa sababu alikumbatia mitandao ya kijamii na akaonya dhidi ya teknolojia ya AI akisema kwamba teknolojia kupita kiasi ni hatari kwa moyo.”
“Papa alikuwa mtu wa kawaida, alionekana kukwepa kabisa maisha ya kifahari na kuchagua maisha ya kawaida tu na kusema kweli tunaenda kukosa ushawishi aliokuwa nao kote duniani na tunatumai Papa mpya atachukua kutoka kwa Francis na pia atakuwa na athari sawia ulimwenguni kote,” Nyamu alisema.
Kuhusu uwezekano wa Papa mpya kutoka bara la Afrika kwa mara ya kwanza katika historia, Nyamu alisema kwamba ni jambo ambalo kila mtu anatumai litafanyika hivyo, akidai kwamba bara la Afrika sasa liko mbele katika kila sekta.
“Papa Mwafrika litakuwa jambo la kufurahisha sana kwa dunia kwa sababu Afrika sasa hivi ndio kifua mbele katika kila sekta,” Nyamu alisema.
Nyamu pia alimtaja Papa Francis kama kiongozi ambaye hakuwa anapenda mivutano ya kisiasa, akirejelea jinsi alivyozungumzia suala la Urusi kuishambulia Ukraine.
“Namkumbuka Papa Francis kama mtu aliyekuwa papa huria ambaye hakutaka kuegemea upande wowote. Hakuogopa kuzungumzia kuhusu vita vya Urusi na Ukraine lakini pia Israel na Gaza.”
“Nakumbuka wakati mmoja alivutia ukosoaji kwa kusema kwamba Urusi ilichochewa na muungano wa NATO kuishambulia Ukraine na kukwepa kumtaja Vladmir Putin moja kwa moja kama mchokozi,” Nyamu alimkumbuka.
Papa Francis alifariki Jumatatu wiki hii na anatarajiwa kuzikwa Jumamosi.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!