Baba Talisha

TIKTOKER Baba Talisha amekuwa mtu wa hivi punde kuzungumzia kuhusu uozo unaoendeshwa na uraibu wa Kamari katika jamii haswa katika mitaa ya maisha ya chini mijini.

Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Baba Talisha amewashauri vijana – ambao kiuhalisia ndio nguvu kazi ya taifa, kukoma kuwa na fikira kwamba Kamari inaweza kuwa njia ya kujitajirisha.

Mpiga picha huyo alishauri kwamba Kamari hakuna siku itakufanya kuwa tajiri na badala yake itafyonza kile kidogo ulicho nacho, na kuwaasa vijana kufuta program zote za kucheza Kamari kwenye simu zao.

Alitilia mkazo akisema kwamba program za Aviator ndizo ambazo zimeleta madhara makubwa ya kisaikolojia kwa vijana na kuwataka kutumia muda wao vizuri katika kujituma kutafuta riziki kwa njia halali nay a haki badala ya kutegemea Kamari.

“Hakuna njia ya mkato katika maisha, futa hizo program zote za Kamari kwenye simu yangu kijana kisha ujitume. Kwanza hiyo ya Aviator,” Baba Talisha alisema.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Ushauri wa Baba Talisha unajiri wiki moja baada ya bunge la kaunti ya Nairobi kuanzisha mchakato wa kujadili mswada unaolenga kudhibiti masuala ya Kamari haswa kwenye mitaa duni.

Mswada huo unaofadhiliwa na MCA wa Ngara Chege Mwaura unalenga kuweka masharti makali kwa waendeshaji wa maduka ya Kamari mitaani, ambapo ikiwa sheria zitakiukwa, waendeshaji wa maduka ya Kamari wanaweza pigwa faini ya hadi milioni moja au miaka 5 jela.

Madhumuni ya mswada huo kulingana na Chege ni kusaidia kudhibiti shughuli za kamari na michezo ya kubahatisha katika maeneo yasiyo rasmi kando na kusaidia kaunti kubuni nafasi za kazi na kuongeza makusanyo ya mapato.

Waendeshaji wa mashine za michezo ya kubahatisha na wamiliki wa majengo wanamofanyia kazi ndio waathirika wakubwa kwani kaunti inalenga kufanya shughuli hiyo kuwa mradi wa gharama kubwa.

Sheria inayopendekezwa inalenga kuanzisha Bodi ya Kaunti ya Jiji la Nairobi ya Kudhibiti Kamari, Bahati Nasibu na Michezo, ambayo itakuwa na jukumu la kutoa leseni kwa shughuli zote za kamari, michezo ya kubahatisha na bahati nasibu katika kaunti.

Mnamo 2021, marekebisho sawa ya sheria ambayo yalitaka kuzuia kucheza kamari kwa hoteli za nyota tano yalifutwa na mahakama.