Marehemu Elvis Murakana Namenya

Mazishi ya mwanawe Mbunge wa Dagoretti Kaskazini, Beatrice Elachi, Elvis Murakana Namenya, yanatarajiwa kufanyika leo, Jumamosi, Machi 29, 2025, katika kijiji cha Nalepo, Kaunti ya Kajiado.

Elvis, aliyefariki Jumanne, Machi 25, 2025, alikuwa mwanafunzi wa Masomo ya Biashara katika Chuo Kikuu cha Africa Nazarene na alikuwa akisubiri kwa hamu kuhitimu mnamo Juni mwaka huu. Kifo chake kimeacha simanzi kubwa kwa familia, marafiki na jamii nzima.

Shughuli rasmi za kumuaga zilianza Alhamisi, Machi 28, 2025, kwa ibada ya wafu iliyofanyika katika Kanisa la Holy Trinity, Kileleshwa, kuanzia saa nne asubuhi. Baadaye, Ijumaa, Machi 29, 2025, mwili wake uliondolewa katika Lee Funeral Home saa moja asubuhi na kusafirishwa kuelekea kijijini kwao kwa maandalizi ya mazishi. 

Kwa mujibu wa familia, maziko yatafanyika leo kuanzia saa nne asubuhi, ambapo ndugu, jamaa na marafiki wamekusanyika kumpa heshima za mwisho. Familia ilimtaja Elvis kama kijana mwenye ndoto kubwa na aliyejaa matumaini kwa maisha yake ya baadaye.

Elvis alizaliwa Septemba 13, 1998, na leo atapumzishwa rasmi katika kijiji cha Nalepo.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Wakati wa ibada ya kumbukumbu iliyofanyika katika Kanisa la Holy Trinity, Kileleshwa, Ijumaa, Machi 27, Elachi alieleza kwa kina namna ajali hiyo ilivyotokea, akifichua kuwa Elvis alipata jeraha kubwa kichwani lililosababisha ubongo wake kuathirika vibaya.

Kwa mujibu wa Elachi, Elvis alikuwa akirejea nyumbani baada ya kukutana na rafiki yake alipokumbwa na tatizo la gurudumu kutoboka ghafla. Kwa kushindwa kuidhibiti hali hiyo, gari lake liligonga vibaya, na majeraha aliyoyapata yakapelekea kifo chake.

“Nataka kuzungumza na wazazi kuhusu watoto wetu leo. Tuna kizazi kinachoamini kuwa kinaweza kushughulikia changamoto zao peke yao. Wanaweza kuamka muda wowote kusaidiana bila hata kutufahamisha. Watatuambia tu ikiwa hawawezi tena kusuluhisha hali hiyo. Lakini wanasaidiana sana, na mara nyingine hata hatujui kinachoendelea,” alisema.

Mbunge huyo alitumia fursa hiyo kuzungumzia usalama barabarani, hasa jinsi ya kushughulikia pancha wakati wa kuendesha gari.

“Elvis alikuwa tayari amelala saa nne na nusu usiku alipigiwa simu kuhusu kazi fulani. Alienda haraka na kuimaliza. Lakini alipokuwa akirejea, gari lake likapata pancha. Vijana wengi hawajui kuwa gari likipata pancha, hupaswi kabisa kubana breki za dharura. Gari litatereza, na hapo ndipo unaweza kupoteza mwelekeo kabisa. Unachopaswa kufanya ni kushikilia usukani kwa nguvu, kuhakikisha gari linapunguza mwendo polepole, na kumwomba Mungu lisimame salama. Kwa bahati mbaya, Elvis alipata jeraha baya sana—ubongo wake ulitoka mahali pake, na hilo ndilo lililosababisha kifo chake,” alieleza.

Elachi alisimulia pia jinsi alivyomtazama mwanaye akiwa ICU siku ya Jumamosi na kufahamu kuwa hangeweza kupona.

"Sikuambia hata madaktari, lakini nilipomtazama, nilijua tu—anaenda zake," alisema kwa huzuni.

Akimzungumzia marehemu mwanaye, mbunge huyo alisema Elvis alikuwa kijana aliyependa sana kanisa, muziki, na soka. Ingawa alikuwa mtu wa kujitenga, alipenda sana mpira wa miguu, na kadri alivyokua, alipata mapenzi makubwa kwa muziki

"Lakini jambo moja nitawaambia, alipenda sana kanisa hili. Na hata ninapokuja hapa, ukiwauliza watu wa Holy Trinity, sijawahi kuja kama 'Mheshimiwa'," aliongeza.

Elachi alihitimisha kwa kumwomba Mungu amrehemu na kumfungulia Elvis mlango wa mbinguni, ili apate pumziko la milele.