AKOTHEE//FACEBOOK

MJASIRIAMALI na msanii Akothee amejitokeza kimasomaso kutetea baba wa wanawe akisema kwamba wako na kila haki ya kusherehekea mafanikio ya wanao.

Akothee alikuwa anamtetea baba wa wanawe, Jared Okello aliyeonekana kusutwa baada ya kuonekana kwenye hafla ya binti yake na Akothee ambaye alikuwa anatambulisha mpenzi wake kwa wazazi wake.

Akothee alimtetea kutoka kwa wale waliokuwa wakimshambulia, akisema kwamba wazazi wenzake wote wamekaribishwa muda wowote kusherehekea mafanikio ya watoto wao.

Kwa mujibu wa Akothee, wazazi wenzake wanakaribishwa kusherehekea naye mafanikio ya wanao bila kujali kama walimsaidia katika malezi au la.

“Baba watoto wangu wote wanakaribishwa kusherekea mafanikio ya watoto wetu iwe nilifanya peke yangu au tulishirikiana nao. Siwezi kujipa mimba mwenyewe. Baba watoto wangu wana nafasi kubwa katika maisha yangu.  Walinibadilisha kutoka kwa msichana hadi kuitwa "mummy", imeishia hapo,” Akothee alisema.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Alimsifia Okello kwa kuweka msingi bora kwa wanawe licha ya penzi lao kuvunjika baadae na kusema kwamba kwa hilo, hawezi simama kando akiona mwanamume huyo akikosewa heshima kwa njia yoyote ile.

“Sitasimama na kutazama mtu yeyote akimtupia dongo baba wa watoto wangu. Jared Okello Otieno ndiye baba mzazi wa watoto wangu wanne, na hakuna kitakachobadilisha hilo.”

“Mwanamume huyu aliweka msingi wa nidhamu katika familia yetu na alikuwa baba wa mfano kabla mambo hayajabadilika na muungano wetu haujafikia kikomo. Lakini hiyo haimaanishi kwamba yeye ni mtu mbaya au kwamba hatakiwi kusherehekea mafanikio ya watoto wake—hata hivyo! Tunabaki kuwa familia, iliyounganishwa sana, licha ya kwenda njia zetu tofauti. Ninatekeleza jukumu langu kama mama yao, huku nikiheshimu pia uwepo wa mtu ambaye ninawajibika sawa kwake,” Akothee aliongeza.

Wikendi iliyopita, Akothee alijumuika na wanafamilia wake kuhudhuria hafla ya kuhalalishwa kwa uchumba wa bintiye, Fancy Makadia nchini Ufaransa.

Fancy Makadia ambaye jina halisi ni Prudence na mpenzi wake Fairouz walihalalisha uhusiano wao mnano Machi 22 nchini Ufaransa.

Akothee alikanusha kwamba hafla hiyo ilikuwa ya harusi akithibitisha kwamba harusi yenyewe itafuata baadae, huku akionyesha furaha ya subira yake kwa siku hiyo kuu.