Askofu Edward Mwai wa Jesus Winner

Askofu Edward Mwai wa Kanisa la Jesus Winner Ministry amesema kwamba amewasamehe wote waliomshambulia katika kipindi cha juma moja lililopita kufuatia mchango aliopokea kutoka kwa Rais William Ruto Jumapili iliyopita..

Akizungumza wakati wa ibada katika kanisa lake la Roysambu asubuhi ya Jumapili, Machi 9, kiongozi huyo wa kidini alidai kuwa wale waliokuwa wakimshambulia walikuwa wanatumiwa na watu fulani ambao anawafahamu.

Hata hivyo, alisisitiza kuwa ameacha kila kitu mikononi mwa Mungu, akieleza kuwa yeye hapambani na mtu yeyote.

"Yeyote amesema neno lolote mbaya. Ninasema nikiwa katika haya madhabahu, ile mawe yote amenitupia, Mungu awasamehe. Mimi nimewasamehe lakini nimewachia Mungu. Sipambani na mtu yeyote," alisema Mwai.

Askofu huyo alidai kuwa kulikuwa na kundi la watu waliotumwa katika kanisa lake Jumapili asubuhi, na baadhi yao walinaswa wakiwa na simu.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Hata hivyo, alisema kuwa kwa roho ya msamaha, aliomba waachiliwe.

"Lakini watu watakuja kujua kuna Mungu kwa haya madhabahu. Kuna Mungu. Mnanishika. Yule Mungu aliongea hapa akasimamisha maombi Mombasa, huyo Mungu, watajua kuna Mungu mbinguni," alionya.

Mwai alizungumza baada ya wiki moja ya mashambulizi makali kutoka kwa Wakenya kwenye mitandao ya kijamii kuhusu mchango wa Shilingi milioni 20 aliopokea kutoka kwa Rais William Ruto mnamo Machi 2, 2025.

Makumi ya maafisa wa polisi walipelekwa katika Kanisa la Jesus Winner Ministry, mtaa wa Roysambu, Nairobi, siku ya Jumapili baada ya vijana kadhaa kutishia kuingia kwa nguvu.

 

Wakenya walikuwa wameunda hashtag #OccupyJesusWinner ili kuhamasisha maandamano yao ya Machi 9, wakipanga kufikisha ujumbe wao hadi kwenye mimbari ya Askofu Edward Mwai.

 

Hii ni baada ya Rais William Ruto kutembelea kanisa hilo mnamo Machi 2 na kuahidi kuchangia Sh20 milioni kutoka mfukoni mwake kusaidia ujenzi wa kanisa, akiahidi mchango zaidi kwenye harambee ijayo ya kusaidia mradi huo.

 

Polisi walikalia baadhi ya viti kanisani huku wengine wakiwa nje wakiwa wamevalia mavazi ya kukabiliana na ghasia.

 

Wahudumu wa kanisa walikagua waumini waliokuwa wakiingia katika jengo hilo, ambalo sasa limezua utata mkubwa.

 

Polisi waliwahakikishia waliokuwa wakifika katika kanisa hilo kuwa usalama wao ulikuwa umeimarishwa, hata kama baadhi ya Wakenya waliendelea kujipanga kwa ajili ya hatua waliopanga kuchukua.

 

Kamanda wa Polisi wa Nairobi, George Sedah, alisema hatua hiyo ni ya tahadhari kwa ajili ya usalama wa kila mtu.

 

Rais William Ruto alimkaribisha Mwai, mwanzilishi wa Kanisa la Jesus Winner Ministry, Ikulu ya Nairobi mnamo Alhamisi.

Ruto alilisifu kanisa la Mwai kwa kuandaa zoezi la uandikishaji wa vijana kwa mpango wa serikali unaolenga kuwaunganisha na fursa za ajira nje ya nchi.

"Tunashukuru Kanisa la Jesus Winner Ministry kwa kusaidia Mpango wetu wa Uhamaji wa Kazi kwa kuwaandikisha vijana kwa ajili ya kupata ajira nje ya nchi," alisema Ruto.

"Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi hizi tunapopanua fursa za ajira na kipato kwa vijana wetu."

 

Ruto alitaka kujua maendeleo ya ujenzi wa kanisa la Mwai huko Roysambu.

 

Mwai alikuwa amefichua kuwa yeye na mkewe wamekuwa wakipokea jumbe kali, hali iliyowalazimu kununua laini mpya za simu tangu Ruto alipoahidi mchango wake.

 

Mchungaji Mwai aliongeza kuwa yeye hapokei wala kuhesabu sadaka na zaka moja kwa moja.

 

Ruto alithibitisha kuwa Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF) lilimkabidhi Mwai kipande cha ardhi huko Roysambu.

 

"Kwa kuwa mimi ndiye Amiri Jeshi Mkuu, niliwaambia KDF kuwa ardhi hii ni mahali patakatifu, na kanisa litajengwa hapa. Nitashiriki nanyi binafsi kuhakikisha hilo linatimia," alisema Ruto.

 

Hili limezidisha hasira miongoni mwa baadhi ya Wakenya, ambao wameendelea kuhamasishana mitandaoni kuhusu mpango wa kuingia kanisani humo kwa nguvu.