Rais William Ruto akaribishwa Kiminini na Gavana George Natembeya mnamo Machi 8, 2025.

Mazishi ya aliyekuwa mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Wafula Chebukati, yanaendelea hivi sasa katika eneo la Kiminini, Kaunti ya Trans Nzoia, huku viongozi wa kitaifa, jamaa, marafiki, na mamia ya waombolezaji wakikusanyika kutoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi huyo aliyekuwa na mchango mkubwa katika kusimamia chaguzi nchini

 

Miongoni mwa viongozi mashuhuri waliohudhuria ni Rais William Ruto, Waziri Mkuu Musalia Mudavadi, Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula, Spika wa Seneti Amason Kingi, Gavana wa Bungoma Ken Lusaka, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, Katibu wa Usalama wa Ndani Raymond Omollo, pamoja na wabunge kadhaa. Pia, aliyekuwa Waziri wa Afya Susan Nakhumicha ni miongoni mwa waliokuja kuomboleza. 

Chebukati atazikwa katika shamba lake la Sabata, Kitale, Kaunti ya Trans Nzoia. Mwili wake uliwasili katika uwanja wa ndege wa Kitale Alhamisi jioni, Machi 6, 2025, ambapo ulipokelewa na familia, marafiki na viongozi wa kisiasa.  

Mazishi haya yanajiri siku chache baada ya ibada ya kumbukumbu iliyofanyika katika kanisa la CITAM Karen, ambapo familia, marafiki, na viongozi walimsifu Chebukati kwa maisha yake ya maadili na uadilifu katika utumishi wa umma.

Chebukati alihudumu kama mwenyekiti wa IEBC kwa kipindi cha miaka sita, akisimamia uchaguzi mkuu wa 2017, marudio ya uchaguzi wa urais wa mwaka huo, na uchaguzi mkuu wa 2022.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Alijulikana kwa msimamo wake wa kuzingatia sheria, na licha ya changamoto nyingi alizokumbana nazo, alihakikisha kuwa matokeo ya uchaguzi yanatangazwa kwa mujibu wa katiba. 

Katika uchaguzi wa 2022, alikabiliwa na shinikizo kubwa wakati wa kutangaza mshindi wa urais, lakini alisimama imara akisisitiza kuwa tume hiyo ilifuata taratibu zote za kisheria. Hatua yake ilizua mijadala mikali ya kisiasa, lakini wengi walimtambua kama mtetezi wa ukweli na haki. 

Mbali na kazi yake katika IEBC, Chebukati alikuwa mume na baba wa watoto watatu—Jonathan, Emmanuel, na Rachel. Wakati wa ibada ya kumbukumbu jijini Nairobi, familia yake ilimtaja kama baba mwenye nidhamu, upendo, na mshauri mzuri kwao.

 

Emmanuel, mwanawe wa pili, alielezea jinsi baba yao alivyowahimiza kuwa na bidii na kutanguliza maadili maishani mwao. 

"Baba alikuwa mtu wa mpangilio na mwenye msimamo. Alitufundisha kuwa maadili na ukweli ni nguzo muhimu katika maisha," alisema Emmanuel. 

Mazishi ya Chebukati yanaendelea, huku viongozi na waombolezaji wakiendelea kutoa heshima zao za mwisho.

 

Kifo chake mnamo Februari 20 kutokana na mshtuko wa moyo kimeacha pengo kubwa katika sekta ya uchaguzi na utawala wa kidemokrasia nchini.