Mshukiwa alimeza ushahidi

Katika tukio la kushangaza na lisilo la kawaida, mwanaume mmoja nchini Marekani alifikia hatua ya kumeza hereni mbili za almasi zenye thamani ya takribani shilingi milioni 99 za Kenya, akijaribu kuficha ushahidi baada ya kuziiba kutoka duka la kifahari la Tiffany & Co.

Jaythan Lawrence Gilder, ambaye tayari anashtakiwa kwa uhalifu wa zamani, alijifanya mwakilishi wa mchezaji wa mpira wa kikapu wa Orlando Magic ili kupata fursa ya kushika na kuangalia hereni hizo za thamani kubwa.

Mara tu alipowekwa mikononi vipuli hivyo vya thamani kubwa – moja likiwa la karati 4.86 lenye thamani ya KSh 20,640,000, na jingine la karati 8.10 likigharimu KSh 78,625,500 – alikimbia mbio kutoka kwenye duka hilo.

Katika harakati za kuzuia uhalifu huo, mmoja wa wafanyakazi wa Tiffany & Co. alijitahidi kumzuia Gilder lakini aliangushwa na kujeruhiwa vibaya wakati mwizi huyo alipojinasua kwa nguvu na kutoroka. 

Baada ya kutoroka, Gilder alikamatwa kwenye barabara kuu ya Interstate 10, akiwa safarini kuelekea sehemu isiyojulikana.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

 

Wakati polisi wakimpekua, waligundua kuwa hereni hizo hazikuwepo mfukoni mwake wala kwenye mizigo yake.

 

Katika hali ya kushangaza, uchunguzi wa X-ray hospitalini ulionyesha kuwa mwizi huyo alizimeza hereni hizo ili kuficha ushahidi!

 

Polisi sasa wanasubiri ushahidi halisi utoke mwilini mwake kabla ya kuthibitisha upotevu wa vipuli hivyo vya thamani.

 

Hii si mara ya kwanza kwa Gilder kujihusisha na uhalifu wa aina hii. Uchunguzi umebaini kuwa ana waranti 48 za kukamatwa huko Colorado na pia anahusishwa na tukio jingine la wizi katika duka la Tiffany & Co. huko Texas mwaka 2022.

 

Kwa sasa, anakabiliwa na mashtaka ya wizi wa kiwango cha kwanza pamoja na ujambazi akiwa amevalia barakoa, mashtaka ambayo yanaweza kumfanya afungwe kwa miaka kadhaa ikiwa atapatikana na hatia.