MSANII na mjasiriamali wa vyombo vya habari, Alikiba ni miongoni mwa waokoaji kadhaa ambao wamejitokeza na kujitosa kimasomaso ndani ya vifusi vya jengo lililoporomoka jijini Dar es S          alaam kutoa msaada wa uokoaji.

Mkurugenzi huyo wa Crown Media na Kings Music alijumuika na waokoaji wengine usiku wa Jumatatu akiwa amevalia mawanda ya uokoaji.

Alikiba alionekana akizama ndani ya vifusi vya jengo hilo la orofa nne lililoporomoka siku chache zilizopita katika soko kuu la Kariakoo, jijini Dar es Salaam.

Baada ya kufika ndani ya vifusi hivyo ambapo shughuli ya uokoaji imekuwa ikiendelea kwa mwendo wa kujikokota kwa zaidi ya siku 3 sasa, alisema kwamba ni jambo la kusikitisha lakini pia akawapongeza wote ambao wanakesha usiku na mchana kuhakikisha wenzao walionaswa ndani ya vifusi hivyo wanaondolewa, ima hai au wakiwa wamefariki.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

“Kwa nafasi yangu mimi nimeweza kufika katika eneo la tukio na kiukweli kazi inayoendelea hapa ni kubwa sana, na kuna vitu vya kusikitisha lakini vile vile kuna vitu vya kuwapongeza baadhi ya wale wanaofanya kazi kubwa ya uokoaji,” Alikiba alisema.

Aliipongeza serikali ya Samia Suluhu Hassan kwa kile alisema kwamba japo walichelewa, lakini waliweza kufanikisha kuleta wataalamu wa kufanya jambo la kuchimba vifusi ili kuokoa maisha.

“Wananchi ndio kila mmoja ameumizwa na kuguswa na jambo hili lakini hili si jambo la kukurupuka useme unatumia nguvu. Hili linaitaji utaalamu. Kama hatuna elimu ya uokoaji kwa jinsi hili jengo lilivyokaa tutajikuta tunaumiza wengine kwa sababu kuna wengine wapo chini na wanawasiliana na waokoaji.”

Msanii huyo aliwaomba watumizi wa mitandao ya kijamii kupunguza mizaha kuhusu kuporomoka kwa jengo hilo, akisema kwamba mwenyewe ameingia hadi ndani kabisa ya jengo la kushuhudia hali ilivyo tete kwa wale walionaswa.

“Kiukweli hili si jambo la kufanyia mzaha tena kwenye mitandao kama inavyoongeleka. Kuna watu wanaongea taarifa tofauti lakini hapa kluna uangalizi mkubwa sana. Hapa kuna usalama mkubwa umewekwa kiasi kwamba hata ufikaji wangu mimi imekuwa ni mchakato mrefu,’ alisema.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari kutoka nchini humo, kufikia Jumatatu, takribani watu 13 walithibitishwa kufariki katika mkasa huo ambao umetajwa kuwa mbaya na rais Samia Hassan.