Mhadhiri wa chuo kimoja nchini Uganda ametoa onyo kali kwa vijana waliopo chuoni dhidi ya kusikiliza na kutazama wimbo wa Hozambee.

Katika video ambayo imekuwa ikipiga misele katika mitandao ya kijamii, mhadhiri huyo ambaye alikuwa anatoa wosia kwa mamia ya wanafunzi katika ukumbi mmoja aliwaambia kwamba wimbo wa Hozambee si wa kusikilizwa.

Aliwafokea akisema kwamba yeyote anayetazama au kusikiliza wimbo huo hawezi kuwa na fanaka maishani, akiutaja wimbo huo kuwa mbaya.

“Mnajua chenye mnafanya kwenye mtandao, mnatazama kuna wimbo Fulani wa kishetani nchini Uganda, sidhani hata kama kuna mtu yeyote anayetazama wimbo huo atafanikiwa maishani. Wimbo huo ni wa kijinga sana, ni Hozambee…” mhadhiri huyo alisema huku akijaribu kuiga kuuimba.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Mhadhiri huyo alisema kwamba wakati wa ujana wake, hawakuwa wanasikiliza nyimbo za aina hiyo bali walikuwa wamejikita sana katika kusikiliza nyimbo za mapinduzi kutoka Afrika Kusini.

“Mnacheka lakini achene niwaambie, wakati tunakua tulikuwa tunasikiliza nyimbo kutoka Afrika Kusini kuhusu mapinduzi. Tulikua tukiwa wapiganaji. Sasa nyinyi mnasikiliza Hozambee,” aliwasxuta vijana.

Aliendelea mbele akisema jinsi kizazi cha sasa barani Afrika kimepotoka kutokana na ujio wa utandawazi, akisema kuwa hata watoto wa chekechea kutoka nchini Uchina wanafanya mambo ya muhimu kuliko vijana wa vyuo vikuu barani Afrika ambao muda wao mwingi unaishia kwenye mitandao ya kijamii.

“Achene niwaambie, watoto wa chekechea nchini Uchina sasa hivi wanafunzwa jinsi ya kutengeneza midoli, na nyinyi hapa mnaimba Hoozambee. Haya ni maajabu. Hivyo, vifaa vtya kielektroniki mlivyo navyo vinaweza kuwaunganisha na watu wenye akili au kwa watu wanaoimba Hoozambee,” alisema.

Msomi huyo alisema kwamba mambo yanayoendelezwa na vijana katika jamii ya kisasa yanamfanya kujihisi mgonjwa na ndio maana anapenda kuwa mbali na kila kitu.

Wimbo wa Hoozambe uliachiwa takribani miezi 5 iliyopita na msanii Mudra D Viral akimshirikisha D Star na mrembo Shifura kwenye video kama vixen.

Wimbo huo mpaka sasa umetazamwa mara milioni 8.5 kwenye jukwaa la video la YouTube.