Wachezaji wenza wa timu ya taifa ya Uingereza Declan Rice na Cole Palmer wa vilabu vya Arsenal na Chelsea mtawalia huenda wakakosa mechi kubwa inayokuja ya Debi ya London.

Chelsea wameratibiwa kuwakaribisha Arsenal katika uwanja wa Stamford Bridge siku ya Jumapili jioni katika mkutano wao wa kwanza wa msimu wa 2024/25.

Wakizungumza na vyombo vya habari siku ya Ijumaa, makocha wa Arsenal na Chelsea walifichua kwamba Rice na Palmer hawakuwa wamefanya mazoezi yoyote kwa ajili ya mechi kubwa inayokuja.

Kocha wa Arsenal Mikel Arteta aliwaambia waandishi wa habari kwamba bado hawajaamua kuhusu hatima ya kiungo wa kati Declan Rice kwani bado hajashiriki mazoezi.

"Declan Rice bado hajafanya mazoezi na bado hatujui kama atakuwepo dhidi ya Chelsea," Arteta alisema.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Enzo Maresca wa Chelsea pia alisema hivyo hivyo kuhusu mchezaji wao bora msimu uliopita Cole Palmer.

Maresca hata hivyo alidokeza kwamba mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 22 alikuwa akipata nafuu vyema kutokana na jeraha lake na wanatumai kuwa naye katika mazoezi ya Jumamosi.

"Cole Palmer anazidi kuwa bora na bado tuna siku mbili za kujiandaa kwa mchezo. Natumai tunaweza kuwa naye kwa kipindi kimoja kisha tuchukue uamuzi wa mechi ya Arsenal," alisema.

Palmer na Rice walipata majeraha mapema wiki hii, jambo lililozua wasiwasi mkubwa kutoka kwa timu za Arsenal na Chelsea huku wakisubiri kukutana Jumapili.

Wote wawili wamekuwa muhimu sana katika timu zao na litakuwa pigo kubwa kwa vilabu hivyo viwili vya London kama hawataweza kuwa tayari kwa mechi kubwa ijayo.