Siku ya Ijumaa jioni, Rais William Samoei Ruto alitangaza kuwa alikuwa ameshiriki katika mazungumzo ya simu na rais anayeingia wa Marekani Donald John Trump.

 

Katika taarifa yake aliyoichapisha kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii, rais alifichua kuwa katika simu hiyo, alimpongeza rais huyo wa 47 wa Marekani kwa kuchaguliwa tena kwa muhula wa pili.

 

Ruto pia alifichua kuwa walipata nafasi ya kujadili masuala ya manufaa ya pande zote mbili ambayo yatafaidi Kenya na Marekani.

 "

Nimekuwa na mazungumzo ya simu na Rais Mteule wa Marekani @realDonaldTrump. Nilimpongeza kufuatia kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa 47 wa Marekani,” Ruto alisema kwenye taarifa.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

 

Aliongeza, “Tulijadili maeneo yenye maslahi kwa pande zote mbili ambayo yana manufaa kwa wananchi wa nchi zetu mbili, ikiwa ni pamoja na biashara na uwekezaji, usalama na utawala bora.

 

Kulingana na rais Ruto, miongoni mwa mada ambazo walipata kujadili ni misheni ya Haiti ambayo Marekani imekuwa ikishirikiana na Kenya.

 

"Nilimweleza Rais Trump kuhusu Ujumbe wa Kimataifa wa Usaidizi wa Usalama wa Kimataifa unaoongozwa na Kenya nchini Haiti na maeneo yanayoweza kushirikiana na serikali ya Marekani kuhusu mpango huu muhimu wa kutatua migogoro," Ruto alisema.

 

Simu hiyo imekuja siku moja tu baada ya Donald Trump kuthibitishwa kuwa amechaguliwa tena kuwa rais wa Marekani kwa muhula wa pili usiofuatana.

Mnamo Jumatano jioni, Rais Ruto aliungana na viongozi wengine wa dunia katika kumpongeza Donald Trump kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa 47 wa Marekani.

Katika taarifa yake, mkuu wa nchi alibainisha kwamba ushindi wa Trump ni ushahidi wa azimio thabiti la watu wa Amerika kuweka imani katika uongozi wake wenye maono, ujasiri na ubunifu.

"Kwa niaba ya Serikali na watu wa Jamhuri ya Kenya na kwa niaba yangu binafsi, nawasilisha pongezi zangu za dhati kwa kuchaguliwa kwako kama Rais wa 47 wa Marekani," Ruto alisema.

Rais aliongeza kuwa Kenya iko tayari kuimarisha zaidi ushirikiano wake na Marekani katika masuala ya maslahi ya pande zote, ikiwa ni pamoja na biashara, uwekezaji, teknolojia na uvumbuzi, amani na usalama, na maendeleo endelevu.

"Kenya inathamini ushirikiano wake wa muda mrefu na Marekani uliodumu kwa zaidi ya miaka 60 unaokitwa katika maadili yetu ya pamoja ya demokrasia, maendeleo na kuheshimiana," alisema.

Aliongeza, "Tunatazamia kuimarisha ushirikiano wetu chini ya uongozi wako tunapofanya kazi pamoja kutatua changamoto za kimataifa, kukuza amani na usalama na kukuza ukuaji wa uchumi shirikishi kwa manufaa ya watu wetu."