
Mmarekani mwenye asili ya Kenya, Huldah Momanyi Hiltsley ameweka historia kubwa kwa kunyakua kiti katika Baraza la Wawakilishi la Minnesota.
Ushindi huo wa mzaliwa wa kaunti ya Nyamira umemfanya kuwa mwanasiasa wa kwanza mzaliwa wa Kenya kushinda kiti nchini Marekani.
Momanyi alishinda kwa 64.78% ya kura kuwakilisha Wilaya ya 38A ya Minnesota huku akigombea chini ya tiketi ya Chama cha Democratic-Farmer-Labor (DFL).
Wilaya 38A inayojumuisha sehemu za kusini-magharibi mwa Brooklyn Park na Osseo ni eneo lenye watu wa matabaka mbalimbali, na takriban 66% ya wakaazi wanajitambulisha kuwa watu wa rangi tofauti, huku sehemu kubwa yao wakiwa wahamiaji kutoka Afrika.
Momanyi amesema uamuzi wake wa kuingia katika siasa ulichochewa na kujitolea kwake kuinua jumuiya yake na kutetea mahitaji yao katika michakato ya kutunga sheria.
Analenga kushughulikia maswala muhimu yanayoathiri wapiga kura wake, akizingatia makazi ya bei nafuu, ufikiaji sawa wa elimu na huduma ya afya, na kuunda fursa za kiuchumi zinazolengwa kwa idadi tofauti ya watu anaowawakilisha.
Mwanasiasa huyo alizaliwa katika kaunti ya Nyamira mwaka wa 1985 na kabla ya kuhamia Marekani ambako alihudhuria Chuo Kikuu cha Bethel katika jimbo la Minnesota.
Mwakilishi wa Wanawake wa kaunti ya Nairobi Esther Passaris ni miongoni mwa watu ambao wamempongeza Momanyi kwa ushindi wake.
Passaris alitambua ushindi wa Momanyi na kuutaja kama jambo la kujivunia kwa Kenya.
"Ushindi wako wa kihistoria kwa hakika ni chanzo cha fahari kwa Kenya na ushuhuda wa mafanikio ya Wakenya wanaoishi Marekani. Hongera sana!" Passaris alisema.