
Katika msako unaoendelea dhidi ya ulanguzi wa dawa za kulevya katika maeneo ya Kaskazini mwa Kenya, maafisa wa usalama wamefanikiwa kumkamata mwanamke mwingine aliyekuwa akisafirisha dawa za kulevya aina ya cocaine, siku moja tu baada ya mshukiwa mwingine kukamatwa kwa mbinu sawia.
Katika kisa cha hivi punde kilichotokea Aprili 19, mwanamke mwenye umri wa miaka 45 aliyetambuliwa kama Caroline Thiunguri Kabonyi alinaswa akiwa ameficha gramu 414 za cocaine katika sehemu zake za siri.
Mshukiwa huyo alikuwa akisafiri kwa gari aina ya Toyota Probox kuelekea Marsabit alipotiwa mbaroni katika barabara ya ukaguzi ya Odda, kaunti ndogo ya Moyale.
Kulingana na taarifa rasmi ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), Caroline alizua vurugu alipokataa kukaguliwa kama ilivyokuwa kwa abiria wenzake.
“Huku wenzake wakitii maagizo ya maafisa wa usalama, Caroline aliamua kupiga kelele na kukataa kukaguliwa, hatua iliyowafanya wachunguzi wa Moyale kumpeleka katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti Ndogo ya Moyale kwa uchunguzi wa kina,” ilisoma taarifa ya DCI.
Uchunguzi wa kitabibu ulithibitisha hofu ya maafisa hao baada ya mabonge nane ya cocaine kupatikana yakiwa yamefichwa katika sehemu zake za siri. DCI ilisema thamani ya mtaani ya dawa hizo ni takriban Shilingi 1,656,000.
Siku moja kabla ya tukio hilo, mwanamke mwingine Jane Njeri Muigai, mwenye umri wa miaka 28, alikamatwa kwenye basi lililokuwa likielekea Nairobi kutoka Moyale, ambapo maafisa waligundua alikuwa ameficha gramu 294 za cocaine sehemu zake za siri pia.
Katika taarifa hiyo ya awali, DCI ilisema: “Mwendesha basi alionekana mwenye wasiwasi kupita kiasi, hali iliyowafanya maafisa wa kike kumpeleka pembeni kwa ukaguzi wa kina, na hivyo kuthibitisha mashaka yao.”
Wawili hao wamezuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Moyale wakisubiri kufikishwa mahakamani huku maafisa wa kupambana na mihadarati wakianzisha hatua za kisheria dhidi yao.
Tukio hili limeibua hofu kuhusu mbinu zinazotumiwa na walanguzi wa mihadarati, huku idara ya DCI ikiahidi kuendeleza msako mkali kuhakikisha mtandao wa ulanguzi unakomeshwa kabisa.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!