
Maafisa wa polisi kutoka Kituo cha Polisi cha Kamagambo mnamo Jumatano walimkamata mshukiwa wa ulanguzi wa dawa za kulevya na kunasa misokoto 401 ya bhangi katika gari la uchukuzi wa umma lililokuwa likielekea Kisumu kutoka Migori.
Kwa mujibu wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), mshukiwa alikamatwa baada ya wananchi wenye uchungu wa usalama kutoa taarifa kuhusu gari lenye nambari ya usajili KDM 981Z, wakishuku lilikuwa limebeba mzigo haramu.
Katika operesheni ya kijasusi, maafisa wa polisi waliweka mtego na kulizuia basi hilo. Upekuzi wa kina ulifichua mabegi mawili yaliyojaa misokoto 401 ya bhangi, yenye uzito wa kilo 34.4 na thamani ya takriban Sh1,032,000 katika soko haramu.
Kwa maoni ya wengi, dereva wa gari hilo, alidhani alikuwa na ujanja wa hali ya juu. Badala ya kubeba abiria wa kawaida, alipakia wanafunzi pekee, labda akifikiria kuwa safari hiyo haingeibua mashaka. Lakini hesabu zake zilikwama.
"Alifikiria kuwa kusafiri na wanafunzi kungemfanya aepuke mashaka. Lakini wananchi walikuwa macho, na polisi walichukua hatua kwa haraka," DCI walisema katika taarifa.
Taarifa hiyo iliongeza kuwa mshukiwa huyo alijifanya hana hatia wakati wa kukamatwa:
"Alipohojiwa, alidai hakujua kilichokuwa ndani ya mabegi hayo, lakini uchunguzi wetu unaonyesha vinginevyo."
Kwa sasa, mshukiwa anazuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Kamagambo akisubiri kufikishwa mahakamani.
Katika Kenya, bhangi ni dawa haramu chini ya Sheria ya Dawa za Kulevya na Vileo. Mtu yeyote anayekamatwa akisafirisha au kutumia bhangi anaweza kufungwa gerezani kwa muda mrefu au kutozwa faini kubwa.
DCI wamesisitiza kuwa hakuna atakayechukuliwa kwa mzaha katika vita dhidi ya mihadarati:
"Ujumbe wetu kwa wote wanaojihusisha na ulanguzi wa dawa za kulevya ni mmoja: tutawapata, na sheria itachukua mkondo wake."
Idara hiyo imewashukuru wananchi kwa kutoa taarifa muhimu na kuhimiza ushirikiano zaidi.
"Usikae kimya! Toa ripoti kwa DCI kupitia nambari ya bure 0800 722 203. Usiogope!" ilisistiza taarifa rasmi ya idara hiyo.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!