
Mwanamuziki maarufu wa Kenya, Avril Nyambura, amefurahishwa kutangaza kwamba anatarajia mtoto wake wa pili!
Avril alifichua habari hii ya furaha kupitia ukurasa wake wa Instagram, ambapo aliandika: "Hapa twende tena. #GratitudeSpace."
Mashabiki wake na watu maarufu walijitokeza kumpongeza Avril kwa furaha, wakimiminika kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii na jumbe za pongezi.
Avril anaye mtoto mmoja, ambaye ni mvulana alizaa na mtayarishaji maarufu J Blessing.
Mwimbaji huyo alizua wasiwasi mwezi Novemba 2023 baada ya kushiriki picha za uso wake ukiwa na alama za kupigwa, akionekana kudai kuwa mzazi mwenzake alikuwa amemvamia na kumpiga.
Avril aliweka picha hizo kupitia akaunti yake ya Instagram ambayo kwa sasa amezima.
Baadaye,
malkia huyo wa muziki alijitokeza kujieleza na kueleza kwa nini alifunguka
hadharani kuhusu yale aliyokuwa akipitia faragha.
"Siku zote nimekuwa mtu wa faragha sana. Siwezi kamwe kuzungumza kuhusu chochote ninachopitia hata kama ninateswa nacho," alisema Avril.
Aliongeza: "Moyo wangu ni mzito sana hivi kwamba ilinibidi kuuambia ulimwengu mambo yangu. Ndiyo, niliona kejeli kuhusu mimi kustahili kila kitu ambacho nimepitia enzi za uhai wangu na nina hakika kutakuwa na kejeli zaidi, lakini pia niliona jumbe za upendo na usaidizi."
Mwanamuziki huyo aliendelea kueleza kuwa amemsamehe J Blessing kwa yote yaliyotokea kati yao na pia kuwataka mashabiki wake wamsamehe mzazi mwenzake.
"Ninakubali kwamba uhusiano wetu wa miaka saba na safari yetu kama wazazi kwa mvulana mdogo mzuri imekabiliwa na changamoto, na kumekuwepo na migogoro ambayo iliongezeka hadi mapigano. Tunatambua hitaji la mabadiliko na tumejitolea kutafuta usaidizi na kujifunza njia bora za kuwasiliana na kutatua masuala. Lengo letu la pande zote mbili ni kujenga mazingira chanya na kusaidiana zaidi, kukuza uelewano na ukuaji," alisema Avril.
Kwa upande wake, J Blessing alikiri kwamba moja ya picha alizochapisha Avril ni tukio lililotokea mwaka 2022.
Alieleza kuwa walikubaliana kuwa ugomvi wao wa kimwili uliosababisha majeraha kwa pande zote mbili, na alikiri kumpeleka Avril hospitali mara moja baada ya tukio hilo.
"Naomba radhi sana kwa madhara niliyomsababishia Avril au mtu mwingine yeyote. Nina hatia, lakini ningependa kufafanua mambo machache. Karibu mwaka mmoja uliopita, tulikuwa na ugomvi wa kimwili ambapo sote tulijeruhiwa, na siku hiyo, mara moja nilimpeleka hospitali," alieleza J Blessing.
Mtayarishaji huyo aliongeza kusema kuwa yeye na Avril wamekubali kuishi tofauti baada ya tukio hilo lililowahusu.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!