
Aliyekuwa Rais wa Chama cha Wanasheria wa Kenya (LSK), Nelson Havi, ameibua mjadala mkali kuhusu matumizi ya bangi baada ya kutangaza kuwa ataenda mahakamani kupinga sheria zinazoifanya kuwa haramu.
Kupitia ujumbe wake kwenye mtandao wa X mnamo Jumapili, Machi 30, 2025, Havi alisema kuwa hajawahi kuelewa kwa nini mmea wa bangi umeorodheshwa kuwa haramu ilhali ni mmea wa asili uliotolewa na Mungu kwa binadamu.
“Sijawahi kuelewa kwa nini bangi imehalalishwa kuwa jinai. Ni mmea unaoota kiasili ambao Jah alimpa mwanadamu,” Havi alisema.
Havi aliongeza kuwa anapanga kuchukua hatua rasmi kwa njia ya kisheria ili kupinga vipengele vya sheria vinavyoharamisha kilimo, uchakataji, uuzaji na matumizi ya bangi nchini.
Alisema kuwa hatua hiyo inalenga kuondoa vizuizi vya kisheria ambavyo, kwa maoni yake, havina msingi wa haki wala mantiki.
“Nitawasilisha kesi ya kikatiba katika wiki ijayo ili kutangaza kuwa vipengele vyote vya sheria vinavyoharamisha kilimo, uchakataji, uuzaji na matumizi ya bangi ni kinyume cha katiba. Lazima tuweke mambo sawa,” alisisitiza.
Kauli yake imeibua hisia mseto miongoni mwa Wakenya, huku baadhi ya watu wakiunga mkono hatua hiyo kwa hoja kuwa bangi ina faida nyingi za kiafya na kiuchumi, ilhali wengine wakiendelea kuonya kuhusu madhara yake kwa jamii.
Uhalali wa bangi kwa matumizi ya kimatibabu na burudani hutofautiana kati ya nchi mbalimbali. Zaidi ya mataifa 50 yameruhusu matumizi ya bangi kwa namna moja au nyingine, huku angalau sita yakiruhusu matumizi yake kwa burudani.
Barani Afrika, nchi kama Malawi, Afrika Kusini, Rwanda na Zimbabwe zimeruhusu matumizi ya bangi kwa matumizi ya kimatibabu. Afrika Kusini ni miongoni mwa mataifa kama Canada, Georgia, Malta, Mexico na Uruguay, pamoja na majimbo 19 ya Marekani na Australian Capital Territory, ambayo yameruhusu matumizi ya bangi kwa burudani.
Nchini Kenya, mjadala kuhusu uhalali wa bangi umekuwa ukiendelea, hasa baada ya mgombea urais mmoja kuahidi kuhalalisha mmea huo ikiwa atachaguliwa.
Wataalamu wameeleza faida kadhaa za kuhalalisha bangi, ikiwemo faida za kiafya, kiuchumi na kijamii. Bangi ina uwezo wa kutibu maumivu, hasa yale ya neva, kuboresha usingizi, kupunguza dalili za wasiwasi na hata kusaidia katika matatizo ya hamu ya tendo la ndoa.
Kiuchumi, nchi zilizohalalisha bangi zimeona ongezeko kubwa la mapato. Kwa mfano, mwaka wa 2021, jimbo la California lilipata mapato ya takriban dola bilioni 1.3 (Shilingi bilioni 153.2) kutokana na kodi ya bangi.
Pia, tafiti zinaonyesha kuwa kuhalalisha bangi kunaweza kupunguza kiwango cha uhalifu, hasa uhalifu wa magenge. Ripoti katika jarida la River Journal nchini Marekani ilieleza kuwa watu huanza kutumia pombe kwa kiwango kidogo wanapopata bangi kihalali, hali inayochangia kushuka kwa uhalifu.
Zaidi ya hayo, wachumi wanasema kuwa kutekeleza sheria dhidi ya bangi ni gharama kubwa na isiyo ya lazima, kwani rasilimali za polisi zinaweza kuelekezwa katika kupambana na uhalifu sugu kama unyanyasaji wa kijinsia na wizi wa kimabavu.
Havi sasa anatarajiwa kutimiza ahadi yake ya kuwasilisha kesi hiyo na kuweka kwenye mizani mjadala kuhusu nafasi ya bangi katika sheria na jamii ya Kenya.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!