CRIME SCENE

Afisa mmoja wa jeshi la Kenya aliawa Ijumaa, Machi 28, wakati wa misheni ya kulinda amani katika Jamhuri ya Afrika ya Kati (CAR).

Afisa huyo wa Jeshi la Kenya (Kenya Army) ndiye aliyekuwa mwathiriwa pekee katika shambulio hilo. Alikuwa amewasili katika taifa hilo lenye machafuko mnamo Februari kama mtaalamu wa uangalizi wa kijeshi.

Taarifa kutoka ofisi ya msemaji wa Umoja wa Mataifa (UN), iliyotolewa kwa niaba ya katibu mkuu António Guterres, ilithibitisha shambulio hilo.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa mlinda amani huyo aliuawa na washambuliaji wasiojulikana wakati wa doria ya umbali mrefu karibu na kijiji cha Tabane, katika mkoa wa Haut-Mbomou, kusini mashariki mwa CAR.

"Katibu mkuu anatuma rambirambi za dhati kwa familia ya mlinda amani aliyeuawa, pamoja na serikali na watu wa Kenya," taarifa hiyo ilisema.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

"Katibu mkuu anakumbusha kuwa mashambulizi yanayowalenga walinda amani wa Umoja wa Mataifa huenda yakahesabiwa kama uhalifu wa kivita chini ya sheria za kimataifa. Anatoa wito kwa mamlaka za Afrika ya Kati kufanya kila juhudi kuwabaini wahusika wa tukio hili ili wafikishwe mbele ya sheria haraka iwezekanavyo."

Jamhuri ya Afrika ya Kati imekuwa katika hali ya machafuko ya ndani tangu mwaka wa 2012, wakati wanamgambo wa Kiislamu kwa wingi walianza kupambana na wanamgambo wa Kikristo wa Anti-Balaka, hali iliyosababisha maelfu ya vifo na kuwalazimu wengi kutegemea msaada wa kibinadamu.

Mnamo mwaka wa 2013, makundi yenye silaha yaliteka mji mkuu na kumlazimisha rais François Bozizé kutoroka. Baada ya kipindi kifupi cha utulivu mnamo 2015 na kufanyika kwa uchaguzi mwaka wa 2016, mapigano yaliongezeka.

Mazungumzo ya amani yalifanyika mapema mwaka wa 2019 chini ya mpango wa Afrika kwa amani na maridhiano katika CAR, ukiongozwa na Umoja wa Afrika (AU) kwa usaidizi wa UN. Makubaliano yalifikiwa mjini Khartoum na kusainiwa rasmi katika mji mkuu wa CAR, Bangui.

Mwakilishi maalum wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati na mkuu wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kusimamia amani katika Afrika ya Kati (MINUSCA), Valentine Rugwabiza, alilaani vikali shambulio hilo lililofanywa dhidi ya doria ya MINUSCA karibu na kijiji cha Tabane, kilomita ishirini na nne kaskazini magharibi mwa mji wa Zemio, katika mkoa wa Haut-Mbomou.

"Mlinda amani mmoja wa Kenya aliuliwa katika shambulio hili la kikatili lililofanywa na watu wenye silaha wasiojulikana," ilisema taarifa hiyo.

"Mwakilishi maalum ameshtushwa sana na shambulio hili la kinyama dhidi ya walinda amani ambao jukumu lao ni kuwalinda raia. Anatuma rambirambi zake za dhati kwa serikali na wananchi wa Kenya na kueleza mshikamano wake kwa familia ya mwathiriwa."

Kikosi cha dharura kimetumwa katika eneo la tukio ili kuhakikisha usalama.

Alisisitiza kuwa mashambulizi ya namna hiyo dhidi ya walinda amani wa MINUSCA hayatateteresha dhamira ya ujumbe huo kutekeleza wajibu wake wa kuleta amani na utulivu katika Jamhuri ya Afrika ya Kati.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilitoa taarifa Jumapili kulaani shambulio hilo nchini CAR, likisisitiza kuwa mashambulizi dhidi ya walinda amani yanaweza kuchukuliwa kama uhalifu wa kivita, huku likikumbusha pande zote juu ya wajibu wao chini ya sheria za kimataifa za kibinadamu.

Mabalozi walitoa wito kwa serikali ya CAR "kufanya uchunguzi wa haraka kuhusu shambulio hilo kwa kushirikiana na MINUSCA, kuhakikisha uwajibikaji kwa kuwafikisha wahusika mbele ya sheria, na kutoa taarifa kwa nchi husika iliyochangia vikosi vya kulinda amani, kulingana na maazimio ya baraza la usalama nambari 2518 (2020) na 2589 (2021)."

Wanachama wa baraza la usalama walisisitiza kuwa kushiriki katika kupanga, kuelekeza, kufadhili au kutekeleza mashambulizi dhidi ya walinda amani kunaweza kuwa msingi wa uwezekano wa vikwazo.