
MSANII mwenye utata, Chris Embarambamba kwa mara nyingine amekuwa gumzo kwenye mitandao ya kijamii baada ya kutoa wimbo kumuomboleza aliyekuwa mwenyekiti wa IEBC, Wafula Chebukati.
Embarambamba alichapisha wimbo huo kwenye YouTube Jumamosi Februari 22, siku moja tu baada ya familia kuthibitisha kifo cha afisa huyo wa IEBC.
Katika wimbo wake, Embarambamba alimuomboleza Chebukati kama aliyekuwa chanzo cha marais Uhuru Kenyatta na William Ruto kuongoza Kenya.
“Nitoboe siri, haki wallahi Chebukati amelala, amekufa. Ndiye alifanya Uhuru [Kenyatta] akaongoza, mtoto wa Kenyatta, Uhuru akaongoza… akasimama imara, Ruto akaongoza, Amen,” Embarambamba aliimba kwa sehemu.
Aidha, katika vesi ya Pili, mwanamuziki huyo mwenye vimbwanga alisimulia matukio yaliyokumba uongozi wa Chebukati katika tume huru ya uchaguzi na mipaka IEBC, kutoka kwa kupigwa vita na baadhi ya makamishna wake hadi wanasiasa.
Akizua utani katika maombolezo yake, Embarambamba alihoji Chebukati aliiacha wapi familia yake lakini pia namba fiche ya M-Pesa yake.
“Chebukati umeacha wapi familia yako… umeacha wapi PIN yako ya M-Pesa… Chebukati ulipitia mateso na shida nyingi, mara kupigwa IEBC…” Embarambamba aliimba huku akimtuma kuwapa salamu viongozi wengine wa Kenya waliotangulia mbele za haki.
Mwenyekiti huyo wa zamani wa IEBC alifariki mwishoni mwa juma lililopita wakati akitibiwa kwenye hospitali moja jijini Nairobi akiwa na umri wa miaka 63.
Kifo chake kiliwagusa wengi, baadhi ya viongozi wa serikali ya Kenya Kwanza wakitoa wito kwa serikali kumpa buriani ya kishujaa katika mazishi ya kitaifa.
Kauli hizo ziliongozwa na mbunge wa Gatundu Kusini, Gabriel Kagombe ambaye alimtaja Chebukati kama mtu aliyekuwa mwenye misimamo yake asiyeweza tetereka licha ya shinikizo kubwa kutoka kwa pande hasimu kisiasa.
Alisema kwamba Chebukati alisimama imara kuhakikisha taifa halikutumbukia katika dimbwi la machafuko ya baada ya uchaguzi katika uchaguzi mkuu wa Agosti 2022, hivyo kudai haja kubwa ya yeye kupewa buriani ya hadhi ya kitaifa.
“Mimi nasema kwamba Chebukati ni shujaa ambaye anastahili kupatiwa heshima yake na mimi najua hata nchi hii na serikali itampa mazishi ama buriani ya kufaa,” Kagombe alijieleza.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!