WAKUU wa majeshi kutoka mataifa wanachama wa jumuiya ya EAC wamekutana jijini Nairobi kujadili jinsi ya kutatua suala la vita katika mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DRC.
Mkutano huo unawaleta pamoja wakuu wa ulinzi kutoka Uganda, Kenya, Rwanda, Tanzania, DRC, Sudan Kusini na Somalia kuweka mikakati ya kurejesha amani na usalama katika eneo hilo.
Jenerali Muhoozi Kainerugaba wa Uganda amekutana na wenzake akiwemo Charles Kahariri wa Kenya miongoni mwa wakuu wengine wa majeshi ukanda wa EAC.
Mkutano huu unafuatia maagizo ya Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki na SADC uliofanyika Februari 8, 2025, jijini Dar es Salaam, Tanzania.
Viongozi wa kanda waliwapa Wakuu wa Vikosi vya Ulinzi jukumu la kutoa mwongozo wa kiufundi juu ya kusuluhisha mzozo huo, huku kundi la waasi la M23 likiendelea kuteka miji muhimu, ikiwa ni pamoja na Goma na Bukavu.
Mashariki mwa DRC kwa muda mrefu imekuwa ikikumbwa na mzozo, huku makundi mengi yenye silaha, ikiwa ni pamoja na Allied Democratic Forces (ADF), yakizidisha ukosefu wa utulivu.
ADF, asili yake kutoka Uganda, imekuwa tishio la kudumu, licha ya operesheni za pamoja za UPDF-FARDC.
Kulingana na UPDF, uwezo wa ADF umedhoofika kwa kiasi kikubwa, huku mabaki yaliyotawanyika tu yakisalia katika misitu minene ya DRC.
Jenerali Kainerugaba wa Uganda aliandamana na Meja Jenerali James Birungi, Mkuu wa Ujasusi na Usalama wa Ulinzi, pamoja na maafisa wengine wakuu wa UPDF.