
MKURUGENZI Mtendaji katika Shirika la Hakimiliki ya Muziki ya Kenya (MCSK), Dkt Ezekiel Mutua amezua maswali kuhusu mmomonyoko wa maadili nchini Kenya haswa kwa kizazi cha sasa.
Kupitia ukurasa wake wa X, Mutua alihoji ni vipi jamii ya sasa imefika mahali ambapo wanamchukia mtu aliyekufa bila kujali msemo wa kale wa ‘Marehemu hasemwi vibaya’.
Mutua alisema kwamba kizazi cha sasa hakina huruma na heshima kwa marehemu kiasi kwamba hata katika umauti wao, bado wanazidi kumtakia tu kifo bila kujali kwamba ameshakufa.
“Ilikuwaje tukapotoka kimaadili hadi kuwasema vibaya wafu, tuwachukie watu hadi kuwatakia kifo hata wakiwa wamekufa?” Mutua alihoji.
Mutua alisema kwamba jambo hilo lilimuacha akifikiria sana alipoona watu wakimsema vibaya aliyekuwa mwenyekiti wa tume ya IEBC, Wafula Chebukati baada ya taarifa za kifo chake.
Alisema kwamba alisikia maoni hayo yakifokwa katika hafla moja ambayo kinara wa chama cha DAP-K, Eugene Wamalwa alikuwa amehudhuria baada ya kutoa ramirambi zake kwa mwendazake Chebukati.
“Nilikumbana na matamshi ya kusikitisha katika hafla iliyohudhuriwa na aliyekuwa Waziri Eugene Wamalwa ambaye alikatizwa na nyimbo za "Wacha akufe tu" alipotaja kuwa tumempoteza aliyekuwa Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati. Tumepoteza ubinadamu wetu? Tutaipataje tena kama nchi?” Mutua aliuliza zaidi.
Kifo cha Chebukati kulihuzinisha taifa Ijumaa asubuhi baada ya familia yake kutangaza kwamba alikuwa amekufa usiku uliopita wakati wa akipokea matibabu hospitalini.
Hata hivyo, familia iliomba kupewa faragha yao wanapomuomboleza mpendwa wao.
Chebukati alichukiwa na kupendwa kwa viwango sawa haswa kutokana na utendakazi wake akiwa mwenyekiti wa tume ya IEBC kati ya 2017 na 2022.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!