Afisa aliyehusika na kucheza wimbo usio sahihi wa taifa la Kenya kabla ya mechi dhidi ya Uganda katika michuano ya kufuzu kwa FIBA Women's AfroBasket 2025 amepigwa kalamu.

 

Tukio hilo lilitokea Februari 3, 2025, jijini Cairo, Misri, ambapo wimbo huo ulidumu kwa sekunde 19 kabla ya kusitishwa, hali iliyowaacha wachezaji wa Kenya wakiwa na huzuni.

 

Wachezaji wa Kenya walionekana kupinga wimbo wa taifa usio sahihi na kutaka usimamishwe ulipokuwa ukicheza. Wimbo wa taifa usio sahihi ulisitishwa baada ya takriban sekunde 20 na ule sahihi ukachezwa kufuatia pingamizi kali la wachezaji.

 

Siku ya Jumanne, Chama cha Kitaifa cha Mpira wa Kikapu cha Kenya (NBA Kenya) kilitoa taarifa kikieleza kuwa ripoti rasmi kuhusu tukio hilo imewasilishwa kwa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Duniani (FIBA) kwa hatua zaidi.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

 

“Mtu aliyehusika kucheza wimbo wa taifa usio sahihi katika mchezo wa Kenya dhidi ya Uganda katika Mashindano ya kufuzu kwa Afrobasket ya FIBA kwa Wanawake, amefukuzwa kazi na ripoti kuandikiwa FIBA," NBA Kenya ilisema katika taarifa yake.

 

Timu ya taifa ya Kenya (Lionesses) ambayo inanuia kufuzu kwa mashindano ya mwaka huu iliishia kupoteza mchuano huo dhidi ya Uganda, 78-56.

 

Timu hiyo iliendelea na mwanzo wake hafifu siku ya Jumanne, Februari 5, 2025, waliposhindwa na Sudan Kusini 86-69 katika mechi yao ya awamu ya pili ya ligi iliyochezwa Cairo, Misri.

 

Hiki kilikuwa kipigo cha pili kwa Lioness, baada ya kupoteza mchuano wao wa kwanza wa awamu ya makundi dhidi ya Uganda.

 

Mashindano ya Awali ya Mchujo ya FIBA ya Wanawake wa AfroBasket 2025 Zone 5, yaliyoanza Februari 3, 2025, yataendelea hadi Februari 8, 2025, kwenye Ukumbi wa Hassan Mostafa Arena huko Giza, Misri.

 

Mataifa sita—Misri, Kenya, Burundi, Tanzania, Sudan Kusini, na Uganda—yanashindana kwa nafasi inayotamaniwa katika FIBA Women’s AfroBasket 2025, iliyoratibiwa kufanyika nchini Côte d’Ivoire.

 

Lionesses wamepangwa pamoja na nchi mwenyeji Misri, Uganda, Burundi, na Sudan Kusini katika mazingira ya kushinda au-kwenda nyumbani huku wakiwania tiketi ya mchuano wa kuwania ubingwa wa bara hilo nchini Côte d'Ivoire.

 

Mashindano haya yanaendelea huku timu zikijitahidi kupata nafasi ya kufuzu kwa michuano ya FIBA Women's AfroBasket 2025.