LILLIAN Ng’ang’a amejipanda kwenye mgororo wa matusi na watumizi wa mitandao wa X baada ya kutoa rai kwa watumizi wa mitandao ya kijamii kuwakosoa viongozi kwa njia ya heshima.
Katika chapisho lake ambalo lilivutia kauli nyinjgi za matusi, mama huyo wa mtoto mmoja alisema kwamba watu wengi wameifanya kuwa kawaida kuwakosoa viongozi mitandaoni kwa kutumia lugha ya matusi.
Kwa mujibu wa Ng’ang’a, kuwakosoa viongozi kwa kutumia lugha ya matusi kunayeyusha maana halisi ya ukosoaji, na kuwataka kutumia lugha ya heshima katika ukosoaji wao.
“Kutumia lugha chafu na kutowaheshimu wengine si jambo la lazima, kwa kadiri tunavyopaswa kuwawajibisha viongozi wetu. Sambaza ujumbe wako kwa njia ya ukomavu, yenye heshima. Kuongeza matusi kunapunguza kusudi,” Lillian Ng’ang’a alirai watu.
Hata hivyo, rai yake ilipokelewa kwa njia hasi na watumizi wa mitandao huo wa X, baadhi wakilivuta jina lake na kuliburura kwenye matope wakidai kwamba amenunuliwa na viongozi.
Vuta-nikuvute hii inajiri wakati ambapo baadhi ya viongozi haswa wale walioko serikalini wamekuwa wakichuana kwa maneno makali ya watumizi wa mitandao ya kijamii, kwa kile viongozi hao wanadai kwamba vijana wamepotoka kimaadili.
Rais Ruto, ambaye amekuwa mwathirika mkubwa wa hulka ya vijana mtandaoni kumtupia maneno na kauli za kudhalilisha uongozi wake amekuwa akitoa rai kwa wazazi mara si moja, akitaka wazazi kuwapa wanao mafunzo ya maadili mema.
Kwa upande mwingine, waziri mpya wa masuala ya ndani Kipchumba Murkomen ametema moto kwa vijana wanaotumia mitandao ya kijamii kuwadhalilisha viongozi kwamba sheria itawavizia.
Murkomen alisema kwamba si kupotoka kimaadili kwa hali ya juu kwa mtu kutumia utandawazi wa AI kubuni picha bandia ya kiongozi akiwa kwenye jeneza.
Alisema tabia hiyo si ya kufurahikiwa, huku akiwasuta wazazi na viongozi wa kidini kwa kuwakingia kifua wale wanaofanya hivyo.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!