Mwanahabari na mwanaharakati wa Tanzania Maria Tsehai Sarungi aliachiwa huru Jumapili jioni baada ya ripoti kuibuka kuwa ametekwa nyara na watu watatu waliokuwa na silaha katika mtaa wa Kilimani, Nairobi.
Sarungi alichapisha kwenye akaunti yake ya X kuwa yuko salama na akaongeza kuwa angetoa maelezo zaidi juu ya kutekwa kwake siku ya Jumatatu.
Maria Tsehai, mkosoaji mkubwa wa utawala wa Rais wa Tanzania Samia Suluhu, alikimbilia Kenya mwaka 2020, akiomba hifadhi baada ya kukabiliwa na vitisho vilivyoongezeka chini ya serikali ya hayati Rais John Magufuli.
Katika miezi ya hivi karibuni, alielezea wasiwasi wake kwa Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International kuhusu usalama wake, akiripoti tukio ambapo wanaume wawili wasiojulikana walionekana wakimtafuta nyumbani kwake alipokuwa hayupo.
Awali siku ya Jumapili, Shirika la Amnesty International lilisema kwamba mwanaharakati Sarungi alitekwa nyara akiwa nchini Kenya.
Katika taarifa kupitia mtandao wa X, shirika hilo lilisema kwamba Maria alitekwa na wanaume watatu waliokuwa na silaha na ambao walikuwa na gari nyeusi aina ya Noah.
Aidha liliongeza kuwa kisa hicho kimetokea mwendo wa saa tisa na robo mchana katika eneo la Chaka Place, mtaa wa Kilimani mjini Nairobi.
Hii si mara ya kwanza raia wa kigeni kutenkwa nchini Kenya.
Mwezi Novemba mwaka jana mwanasiasa wa upinzani wa Uganda Kizza Besigye alitekwa mjini Nairobi na watu wasiojulikana na kurejeshwa nyumbani.
Wakimbizi wannne Wa Kituruki pia walitekwa na kutimuliwa kwa lazima hadi Ankara, ambako walikabiliwa na tuhuma za kula njama dhidi ya Rais Recep Tayyip Erdogan.
Comments 0
Sign in to join the conversation
Sign In Create AccountNo comments yet. Be the first to share your thoughts!