CASSYPOOL amefichua kwamba atakuwa katika kinyang’anyiro cha ugavana wa kaunti ya Nairobi katika uchaguzi wa mwaka 2027.


Akizungumza na waandishi wa Habari, Cassypool alisema kwamba yeye haoni mshindani yeyote wa nguvu kando na gavana wa sasa Johnson Sakaja na mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino.


Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Babu Owino amekuwa akitajwa kwa muda sasa kama mmoja wa wanasiasa wanaopiga njaramba kujitosa kwenye dimba kuwania ugavana wa Nairobi katika uchaguzi mkuu ujao.


Cassypool hata hivyo alionesha Imani yake ya kuwabwaga wawili hao katika kile alichokitaja kuwa ni ‘mapema asubuhi’.


Hata hivyo, alipuuzilia mbali ushindani kutoka kwa mtu mwingine yeyote, akimtaja msanii Bahati kama asiye na athari hata chembe kwenye ushindani.


“Mimi nasimama gavana Nairobi, saa kumi na mbili asubuhi nitakuwa nimemaliza hiyo shughuli nimetandika kina Babu Owino, nimetandika Johnson Sakaja. Lakini Bahati si mtu unahesabu katika mbio za ugavana, kwanza ni nani huyo anaitwa Bahati? Naongea kuhusu Babu Owino atakayekuwa kwenye kinyang’anyiro, naongea kuhusu Sakaja. Watu ambao nitatandika katika mbio za ugavana Nairobi,” Cassypool alisisitiza.



Iwapo Bahati atakuwa kwenye kinyang’anyiro cha ugavana Nairobi, basi haitakuwa mara yake ya kwanza kujitosa kwenye siasa.


Itakumbukwa msanii huyo aliwania ubunge wa Mathare katika uchaguzi wa Agosti 2022 lakini akashindwa vibaya na kumaliza katika nafasi ya 3 nyuma ya mshindi kutoka chama cha ODM na nambari mbili kutoka UDA.


Licha ya Cassypool kufichua kuwa atawania ugavana, haibainiki kama anasema kweli ama ni moja ya mbinu zake za kutafuta kiki, kwani amezoeleka na wengi kwa kauli ambazo mwisho wa siku huishia kutotekelezeka.