MSANII Kevin Bahati Kioko alikuwa na wakati mgumu kutoa maelezo kwa wanawe wa kike sababu ya kuvalia mavazi ya kike hali ya kuwa yeye ni baba.

Katika klipu fupi aliyoichapisha kwenye ukurasa wake wa Instagram, Bahati alionekana akiwa amevaa vazi la kike – linalokisiwa kuwa la mkewe, Diana Marua.

Ghafla mabinti zake, Mueni na Heaven wakamfumania akirekodiwa huku akijishebedua kama mwanasosholaiti kwenye vazi hilo.

Mshangao katika nyuso za mabinti wake ulishamiri, wote wakishindwa kujizuia kufahamu ni nini kimemkuta baba yao.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Bahati alijaribu kuwaeleza mabinti hao kuwa alikuwa anafanya hivyo, si kwa kupotoka kimaadili bali ni kwa ajili ya kutengeneza maudhui tu, lakini nyuso za mabinti hao zilionekana kutokubali maelezo yake.

“Nani atawaelewesha Watoto wangu kuwa Baba anatengeneza Maudhui tu???!!!” Bahati aliandika kwenye video hiyo baada ya maelezo yake kushindwa kuwashawizi mabinti zake.



Mabinti hao walicheka na kuanguka chini huku baba yao akijaribu kuwashawishi kukubali kwamba ni maudhui tu anajaribu kutengeneza na si vinginevyo.

Baada ya kicheko cha muda, mabinti zake walipata nguvu ya kuinuka na kumkabili baba yao na maswali, “Baba kusema ukweli sasa hiki unachofanya ni nini?”

Binti Mueni aliibua kumbukumbu kwamba hii si mara ya kwanza kumuona babake akiwa katika mavazi ya kike kwani wakati Fulani alimuona akiwa amevalia viatu vya visigino virefu na kumalizia kichwani na wigi la kike.

Safari hii kando na vazi la kike, Bahati alijipodoa kwenye midomo na kubeba mkoba wa kike, katika kile mkewe alisikika akisema ni “kumalizia muonekano wa kike mia fil mia.”



Bahati si mtu maarufu wa kwanza nchini kuonekana katika mavazi kinyume na jinsia yake.

Wengine wengi tu akiwemo Kinuthia, Eric Omondi, Mtumba Man … wamekuwa wakizua mjadala pevu wanapovalia mavazi ya kike na hata kujipodoa kama wanawake.

Kwa wakati mmoja, mchungaji Robert Burale aliwafokea na kuwakemea wanaovalia mavazi kinyume na jninsi yao, haswa wanaume akiwasuta kuwa wanapotosha jamii kimaadili.

Katika mazungumzo na Obinna mnamo Aprili mwaka huu, Burale alisema kwamba kuvalia nguo za kike hali ya kuwa wewe ni mwanaume kwa kauli kwamba “ni unga unatafuta” ni kujikosea heshima, lakini pia kudumisha jinsia ya mtoto wa kiume.



"Pia anahitaji kufundishwa. Kwa nini avae kama mwanamke, akicheza kwenye mitandao ya kijamii? Anahitaji kuambiwa ukweli. Huwezi kwenda kufanya twerking, na wewe ni mwanaume. Anahitaji kuambiwa ukweli," Burale alisema.

Burale ni mmoja kati ya wachungaji wachache ambao katika mahubiri yao aghalabu, hukemea vitendo vinavyoonekana kuenda kinyume na jinsia ya mtu, akisema kwamba ni wajibu wake kufungua macho ya kizazi cha sasa ambacho anahisi kimefumbwa na wimbo la mitandao ya kijamii.