MWANASOSHOLAITI na mfanyibiashara wa bidhaa za urembo Huddah Monroe kwa mara nyingine tena amejibu kuhusu uvumi wa kuwa mwanachama wa iluminati.

Akizungumza na mashabiki wake kupitia kipindi cha maswali na majibu kwenye Instagram, Monroe aliulizwa na shabiki mmoja kutangaza msimamo wake ikiwa ni mwanachama wa iluminati au la.

Monroe alijibu waziwazi kwamba angekuwa kwenye jumuiya hiyo asingekuwa anahangaika kuzumbua riziki usiku na mchaka siku 7 za wiki.

Kauli yake ilitengua dhana kwamba wanaokuwa wanachama wa iluminati huwa na ukwasi wa ghafla ambao hawakuufanyia kazi.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

“Wewe ni mwanachama wa iluminati?” shabiki alimuuliza.

“Natamani ningekuwa, kwa sababu nisingekuwa nafanya kazi kwa bidii hivi,” Monroe alijibu.

Hii si mara ya kwanza kwa suala la kuwa kwenye iluminati linaibuliwa dhidi ya mfanyibiashara huyo.

Miezi kadhaa iliyopita alipobadilisha picha ya utambulisho kwenye ukurasa wake wa Instagram, Huddah alilazimika kuwafafanulia mashabiki wake maana ya picha hiyo ambayo wengi waliihusisha na nembo ya jumuiya ya iluminati.

Monroe alisema kuwa picha hiyo yenye jicho ni jicho lenye nguvu kuu linalomuangalia muda wote kutoka juu.

Pia mwezi Julai mwaka huu, Monroe aliwashangaza wengi alipokiri kwamba akatakiwa kuchagua kati ya Ukristo na iluminati, angechagua iluminati akiwatuhumu Wakristo kwa kuwa vigeugeu na waongo.

Kupitia mfululizo wa hadithi za Instagram, Huddah Monroe, ambaye wakati huo alikuwa amefichua kuwa ana mipango ya kufungua kanisa, aliwashutumu waumini wa kanisa kuwa waongo.

"Kwa wakati huu, ningechagua Illuminati kuliko Mkristo. Waumini wote hawa ni waongo,” alisema.

"Wote huenda kanisani na pesa zetu hupotea."

Awali, mwanasosholaiti huyo ambaye mara nyingi huonekana jijini Dubai alifichua kwamba ana mpango wa kurejea nchini Kenya mwaka 2026 na kuanza mchakato wa kueneza injili.

"Kwa wale wanaoshangaa, ninarudi 2026 kufungua kanisa. Roho mtakatifu ndiye aliyeniita,” akaeleza.

“Kama wewe ni mchungaji chipukizi au nabii, nitakuajiri shikilia Biblia yako na uisome. Waislamu pia wanakaribishwa kwenye ‘Huddah Prosperity Church’. Mahali panapokupa utulivu wa akili na kubadilisha maisha yako kutoka 0-100,” Monroe alitangaza.

Huddah Monroe alishiriki misheni na kauli mbiu ya kanisa na kusema kanisa lake litaleta mabadiliko chanya na ushirikiano wa vijana.

“Kauli mbiu ya Kanisa la Huddah Prosperity ‘Kubadilisha Maisha’ au inaweza kuwarudisha vijana kwa Mungu na mafundisho yake. Tutajadiliana,” Monroe aliongeza.