AFISA mkuu mtendaji wa Jumuiya ya hakimiliki ya muziki ya Kenya (MCSK), Dkt Ezekiel Mutua amevunja kimya chake, siku moja baada ya kuenezwa kwa barua inayodai kuwa amesimamishwa kazi.

Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Mutua alichapisha taarifa ndefu akipuuzilia mbali taarifa hizo kama uvumi feki unaonuia kuchafua jina lake.

Dkt Mutua alisema kwamba watu wanaodai kuwa wanachama wa kamati kuu ya MCSK wote hawajui na kufichua kuwa tayari yuko ofisini kushughulikia uvumi huo alioutaja kama propaganda mbaya.

Mutua alisema kwamba wikendi iliyopita alikuwa nchini DRC na baadae kurejea nchini kwa shughuli nyingine na hivyo alishangazwa sana kuona uvumi mitandaoni kwamba amesimamishwa kazi.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

“Kwa hiyo ilishangaza kwangu kujua baadaye kwamba nilipokuwa nikishughulika sana kutekeleza jukumu langu kama Mkurugenzi Mtendaji wa Jumuiya ya Hakimiliki ya Muziki ya Kenya mtu fulani alikuwa akieneza propaganda mbaya kuhusu madai ya kuachishwa kazi kwangu, au ilikuwa ni kusimamishwa kazi?” Mutua alihoji.

CEO huyo alithibitisha kwamba bado yuko ofisini kama afisa mkuu mtendaji wa MCSK, akiwataka wanablogu wanaoeneza uvumi wa kusimamishwa kwake kazi kufanya haki kwa kutembea ofisini kupata ukweli kamili kutoka kwake.

Hata hivyo, Mutua alithibitisha kwamba kuna vuta-nikuvute katika uongozi wa MCSK lakini akasema kuwa mzozo huo haufikii cheo chake bali unaishia katika vyeo vya wanachama waliochaguliwa tu.

“Ni kweli kwamba kuna mizozo ya uongozi katika MCSK lakini inagusa tu Wakurugenzi walio na nyadhifa zisizo za watendaji waliochaguliwa. Mkurugenzi Mtendaji na wafanyakazi hawajachaguliwa na kuna taratibu za wazi za hatua za kinidhamu,” alisema.

Mutua alifichua kwamba leo alifaa kuwa na mkutano nje ya ofisini lakini ikambidi kusalia ofisini ili kumaliza kabisa ukungu unaozingira uvumi wa kusimamishwa kwake kazi, akisema kuwa tayari amewaarifu mawakili wake kuchukua hatua madhubuti za kisheria.

“Nilipaswa kuwa kwenye mikutano nje ya ofisi leo lakini ilinibidi kughairi na kubaki ili kushughulikia propaganda fulani. Kama msemo unavyokwenda, "kitu pekee cha lazima kwa ushindi wa uovu ni kwa watu wema kufanya chochote." Nimewaelekeza wanasheria wangu ipasavyo,” Mutua alikiri.